Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye

Iringa.
 Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye amewataka Watanzania kupambana na kuhakikisha suala la udini unaoanza kuota mzizi katika nchi hii linafanyiwa kazi na kwamba likiachwa hivyo nchi itakwenda pabaya.
Kauli ya Sumaye ni muendelezo wa kauli za viongozi mbalimbali wa taasisi za dini na wanasiasa kutaka kuhakikisha kila Mtanzania analinda amani na utulivu nchini.
Akizungumza wakati wa hafla ya harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) linalojengwa ndani ya Chuo Kikuu cha Tumaini mkoani hapa, Sumaye alisema katika vita ya udini siku zote hakuna mtu anayeweza kushinda.
“Taifa hili kwa sasa limekosa uzalendo, watu wamekuwa wakifanya matendo mabaya na yasiyo mpendekeza ya Mungu …leo imefikia wakati watu wameanza kubaguana kwa nyazifa zao, mahali walipo na sasa suala hili la udini” alisema Sumaye na kuongeza:
“Hili linapaswa kufanyiwa kazi haraka kwani likiaacha liendelea litaliingiza taifa kwenye hatari isiyoweza kuzuilika,” alisema.

Sumaye aliwataka viongozi wa dini kufundisha watu wao upendo kutoka kwa Mungu akisisitiza kuwa katika vitabu vitakatifu ndipo yanakokatazwa mambo yasiyompendekeza Mungu.

Akizungumzia kuhusu vijana Sumaye alionya tabia iliyojengeka ya Watanzania kushindwa kujituma wakati wa utendaji kazi akisema hali hiyo katika kipindi hiki cha biashara huria Watanzania wengi wanaweza kupoteza sifa zao licha ya kuwa na sifa za kufanya hivyo.

“Mungu hapendi uvivu wala umasikini,anapenda utajiri na matajiri lakini uwe wa haki, hapendezwi na wizi,ufisadi …mali ya ufisadi ni hatari kwani inaweza kuchochea mambo mabaya kutendeka katika nchi yetu,” alisema.