Katika mkutano na waandishi wa habari mjini Nairobi, waziri wa mambo ya ndani ya nchi wa Kenya alitupilia mbali swala kwamba serikali ya Kenya ingefaa kuzindukana baada ya kupata habari mapema kwamba kuna uwezekano wa shambulio kubwa la kigaidi kutokea katika mji mkuu.Waziri Joseph Ole Lenku alilitoa maanani swala hilo la mwandishi wa BBC na kusema kuwa taarifa za ujasusi, yaani intelijensi, ni swala la serikali:"Sifikiri kama weye ndie wa kuniambia mimi nini serikali ingefaa kusema au la.
Kuhusu taarifa na ujasusi wetu, hilo halijakuhusu.

Tumeonesha hapa, na tunaendelea kusema, kuwa taarifa za ujasusi zitabaki hivohivo, habari za ujasusi; na hatutasema hadharani.
Kwa hivo intelijensia yetu ni siri na siyo kitu tutakizungumza hadharani."
Waziri huyo wa Kenya piya alizilaumu nchi, pamoja na Marekani, ambazo zimeonya wananchi wao wasiende Kenya.
Alisema ilani kama hizo hazihitajiki na wala si za kirafiki na hazisaidii katika kupambana na ugaidi wa kimataifa.
Alisema Kenya haitawaachia magaidi kuwatia khofu watu wa Kenya.