KWAKO,
Nasibu Abdul ‘Diamond’. Pole na kazi na mihangaiko ya hapa na pale. Najua uko bize sana na shoo za kila kukicha. Siyo mbaya, ndiyo maisha, maana bila kazi inakuwa siyo maisha tena.
Muda mrefu sana hatuwasiliani... nasikia siku hizi unapokea simu kwa nadra sana! Hata hivyo, siyo lengo langu kuzungumzia hayo. Ni kitambo kidogo hatujakutana kwenye barua.
Naamini leo ni sahihi zaidi kukufikishia ujumbe huu. Hata kama kuna mengine niliyotaka kuzungumza nawe, lakini kuna jambo ulilofanya, limenifanya niweke mengine yote pembeni kwanza.
Diamond, siri ya mafanikio ya binadamu yapo katika utoaji. Hapo kuna mara mbili; kutoa kwa wahitaji ambao hawajiwezi au kutoa kama shukrani kwa wanaochangia mafanikio yako!
Mwaka jana katika Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni, Dar ulifanya Tamasha la Krismasi na Ngololo ambapo pia uliwashindanisha watoto kucheza wimbo wako wa Number One ambao ndani yake kuna kionjo cha Ngololo.
Ahadi yako kwa washindi ilikuwa ni kuwasomesha watoto hao katika shule bora kama zawadi kwao. Ilikuwa ahadi nzuri sana kwako, maana wote walikuwa wakisoma katika shule za kawaida a.k.a St. Kayumba.
Ile ilibaki kuwa ahadi tu... wengi waliamini yalikuwa maneno ya kujipaisha. Kitendo chako cha kutimiza ahadi hiyo Januari 21, mwaka huu kwa kuwapeleka hao watoto katika Shule ya Kimataifa ya Afrika Mashariki (East Africa International School), iliyopo Mikocheni, Dar kimekuongezea heshima kubwa kwenye jamii.
Hii imeonesha ni kwa namna gani umetambua na kuthamini elimu. Ni vigumu sana kwa msanii mwingine kufunika rekodi hii, hata kama mwingine akija kufanya, atakuwa ameiga kutoka kwako.
Nasikia wanafunzi hao, mmoja ameingia darasa la nne  na mwingine la tano na wote kwa pamoja umeahidi kuwasomesha mpaka watakapomaliza darasa la saba.
Hongera sana bwana mdogo. Hapo umeonyesha ukomavu wa fikra wa hali ya juu. Jambo hili liwe fundisho kwa wasanii wenzako. Kumbe mnaweza kufanya mambo makubwa kwa jamii na mkajenga heshima.
Bila shaka yoyote, utakuwa umejiongezea mashabiki luluki kwa tendo hilo ambalo pengine kuna msanii hakuwahi kulifikiria. Hapo tegemea mafanikio katika kazi yako, maana umerudisha sehemu ya pato lako kwa mashabiki wako.
Hongera sana. Nadhani nikuache ufanye kazi, lakini sasa Diamond, mbona hupokei simu za waandishi kamanda? Nasikia wifi yetu  amekubana... ni kweli? Hayo tutaongea siku nyingine ila kwa hili la kuwalipia madogo ada, chukua tano!
Yuleyule,
 
Mkweli daima, 

Joseph Shaluwa