Mafuriko yakosesha makazi watu 2500 Moro. Wengine 17 wafa Mtwara, Singida.
Ni maafa, maafa maafa.Ni majonzi na masikitiko makubwa yaliyojitokeza katika kipindi cha siku saba zilizopita  kwa Watanzania baada ya kushuhudia zaidi ya Watanzania 17  wakipoteza maisha yao, kupoteza makazi huku wengine wakibaki majeruhi.
Ndani ya siku hizo saba, kumetokea maafa makubwa matatu ambayo ni pamoja na vifo vya wanafunzi wanne mkoani Mtwara, abiria 13 katika ajali ya gari Singida na mafuriko makubwa yaliyotokea juzi katika Mkoa wa Morogoro.
Katika matukio hayo, taarifa zinaonesha kuwepo kwa uzembe uliosababisha na madereva barabarani; uzembe wao umesababisha kupoteza maisha ya watu wasiokuwa na hatia pamoja na mali zao.
Mafuriko Morogoro
Licha ya utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa kutoonyesha kwamba kuna hali ya hatari ingetokea, mvua kubwa zimenyesha na kusababisha mafuriko yaliyotokea Mkoani Morogoro. Tukio hilo limewatesa pia Watanzania kutokana na taarifa kuonyesha kuwa zimewaacha zaidi ya watu 2500 bila makazi, huku kukiwa hakuna mkakati wa haraka kuwasaidia wale walioathirika.
Baadhi ya watu waliokumbwa na mafuriko hayo wanalia kwamba hali ya maisha yao imeharibika ghafla na hawajui la kufanya, kwani baadhi yao wanadai hawana vyakula wala nguo za kubadilisha.
Mafuriko yalivyotokea Morogoro
Katika tukio la mafuriko, mvua hizo zilizotokea juzi katika Kata ya Dumila, Kilosa mkoani Morogoro, zilikuwa kubwa hatua iliyosababisha daraja la mto Mkundi linaloziunganisha Wilaya za Kilosa na Mvomero kuvunjika.
Mvua hizo zilianza kunyesha alfajiri, muda mfupi zilisababisha maafa makubwa ikiwamo kuharibiwa kwa makazi ya watu, majengo ya Serikali zikiwamo shule, vyuo, mahakama na mashamba.
Kutokana na mvua hizo, wananchi walionekana kukumbwa na taharuki kubwa kiasi cha baadhi yao kutawanyika ovyo, wakishindwa kujua la kufanya. Baadhi ya wakazi hawakujua mahali pa kujihifadhi kwa wakati huo baada ya nyumba zao kuharibiwa, mali zao sanjari na mazao kusombwa na maji. Maji yalionekana kusambaa kwenye vijiji mbalimbali vinavyozunguka mto huo na kuwalazimisha baadhi ya watu kupanda kwenye miti na juu ya nyumba kwa lengo la kujiokoa, huku wengine wakitapata kwenye maji kusaka kujiokoa baada ya kusomwa na maji ghafla au njia walizokuwa wakipita kuvamiwa na maji yaliyokuwa yakitiririka kwa kasi.
Baadhi ya watu walikutwa na mafuriko hayo wakiwa mashambani na walipozidiwa na nguvu ya maji walijiokoa kwa kushikilia vitu mbalimbali ikiwamo miti, huku baadhi yao wakipoteza vitu mbalimbali vikiwemo majembe,  na hata nguo walizokuwa wamevaa, hasa kwa wanawake ambao wengi wao huvaa nguo nyingi kama vile gauni khanga au nyinginezo za kujitanda kwa juu. Polisi waliofika eneo hilo kwa ajili ya uokoaji walilazimika kuomba helikopta kutoka makao makuu ya jeshi hilo, Dar es salaam ili kuwaokoa watu waliokuwa kwenye paa za nyumba na kwenye miti iliyokuwa imezungukwa na maji.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa morogoro, Joel Bendera alitaka kuwapo kwa uvumilivu wakati Serikali ikiendelea na taratibu za kuwaokoa walioko juu ya miti na kutoa misaada mingine kwa waliokumbwa na mkasa huo.Diwani wa Kata ya Magole, Juma Rajabu Chewe anasema katika tukio hilo maiti ya mtu ilionekana ikielea kwenye maji yaliyokuwa yakipita kwa kasi.Chewe alisema maiti hiyo ilionekana ikielea eneo la Mateteni na kwamba taarifa zilitolewa polisi ili aopolewe, hata hivyo bado hajatambuliwa.
Ajali ya Wanafunzi Mtwara
Tukio lingine kubwa na la kusikitisha ni pamoja na gari aina ya Marcedes Benz Namba T174 ead  ambayo iliwagonga wanafunzi wanne na kufariki hapo hapo huku wengine 51 wakijeruhiwa.
Wanafunzi hao ni wa Shule ya Sekondari ya Mustapha Sabodo iliyopo kijiji cha Msijute, Mtwara mjini, waligongwa na gari hilo juzi asubuhi wakati wakikimbia mchakamchaka katika barabara ya Dar es Salaam-Lindi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Zelothe alisema tukio hilo limesababishwa na dereva wa gari hilo Baraka Mgengwe kuendesha mwendo wa kasi akitokea Mtwara.
Watu 13 wafariki dunia kwa ajali Singida
Siku nne zilizopita, ajali nyingine kubwa mkoani Singida ilitokea katika eneo la kijiji cha Isuna wilayani Ikungi,Mkoa wa Singida baada ya magari mawili ambayo ni gari kubwa na Noah hatua iliyosababisha watu 13 kufariki dunia pale pale huku wengine 16 wakibakia majeruhi.
Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida,Godfrey Kamwela anasema  chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi na uzembe wa madereva barabarani.
Pamoja na kukithiri kwa ajali hizo za barabarani mpaka sasa jeshi la Polisi limeonekana kuelemewa na changamoto ya kudhibiti usalama barabarani kutokana na madai mbalimbali hasa ya kukithiri kwa rushwa.
Baadhi ya watu walioongea na gazeti hili wamemshauri Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani, kujithamini na kuwaangalia upya namna vijana wake wanavyofanya kazi nchini.