Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akijibu maswali ya papo kwa hapo  Bungeni, mjini Dodoma jana. Picha na Edwin Mjwahuzi
                                                                       Dodoma.
 Waziri Mkuu, Mizengo Pinda jana alifanikiwa kutuliza hali ya hewa bungeni baada ya kutoa mapendekezo yaliyoungwa mkono na pande zote zilizokuwa zinavutana kuhusu kupitisha baadhi ya vifungu vya Kanuni za Bunge la Katiba.
Katika mapendekezo yake yaliyoungwa mkono na Naibu Katibu Mkuu wa CCM -Zanzibar, Vuai Ali Vuai, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Pinda alisema: “Nataka kuwaomba wenzangu wote kwenye maeneo hayo (yenye malumbano) tukiwa tunayapitia kama hatutaelewana tuyaache kwa muda na kumwomba Mwenyekiti aunde timu ya watu wazima na wenye busara wajaribu kuyatazama. “Tujadiliane, tushindane kwa lugha za staha, tusitumie lugha inayoweza kukasirisha. Isiwe mimi nimesema, mimi nimesema...”
Waziri Mkuu, aliwataka wajumbe wajiepushe na lugha za kuudhi ambazo zinaweza kukwamisha upatikanaji wa Katiba Mpya.
Pinda alilazimika kuingilia kati baada ya kutokea mgawanyiko mkubwa wa namna ya kupiga kura kupitisha vifungu vya rasimu.
Akiunga mkono ushauri huo, Mbowe alisema Bunge limejaa hisia za hofu ndani na nje, jambo ambalo linatia wasiwasi wa kupatikana kwa Katiba Mpya. Alisema iwapo wajumbe watashirikiana na kuweka kando masilahi ya vyama, idadi yao katika makundi, Katiba inaweza kupatikana.
Vuai alionya kuhusu matumizi ya lugha za kuudhi huku Profesa Lipumba akiwataka wajumbe kuzingatia masilahi ya Taifa kama alivyoagiza Rais Jakaya Kikwete na kutengeneza Katiba ya Watanzania wote bila ya kujali masilahi binafsi.
Upigaji kura bungeni vita
Awali, mjadala wa utaratibu wa upigaji kura katika Bunge hilo ulichukua sura mpya baada ya kudaiwa kuwapo ushawishi unaohusisha utoaji wa bahasha ili kutaka kuungwa mkono katika misimamo inayokinzana.
Habari zilizopatikana zilidai kuwa watuhumiwa katika sakata hilo ni baadhi ya wajumbe ambao ni mawaziri na mbunge mmoja wa CCM. Vigogo hao wanadaiwa kuwashawishi wajumbe ambao hawatokani na vyama vya siasa ili kupitisha agenda ya kura ya wazi kirahisi.
Akiandika kwenye ukurasa wake wa Facebook, Mjumbe wa Bunge hilo, Julius Mtatiro ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa CUF, alisema: “Jaribio la kuzuia kura ya siri limechukua njia za aibu, baada ya CCM kutumia fedha kushawishi wajumbe.”
Katika ujumbe huo ambao alikiri kuuandika, Mtatiro aliwataja wajumbe watatu ambao ni mawaziri kuwa waliwakaribisha wajumbe kwenye makazi yao na “kuwaandalia chakula cha kutosha, vinywaji vya kutosha na viburudisho vingine, huku wakipewa bahasha za nauli baada ya vikao hivyo vya siri.” Mmoja wa waliotajwa ni Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe aliyedaiwa kuwaalika wawakilishi wa wafugaji na kuwapa chakuka na bahasha.
Akijibu tuhuma hizo, pamoja na kukiri kuwakaribisha baadhi ya wajumbe na kula nao chakula, alikana tuhuma za kuwahonga ili waunge mkono msimamo wa chama hicho. Alisema Mtatiro amemdhalilisha, hivyo anawasiliana na mwanasheria wake ili kumfikisha mahakamani.“Siwezi kumuacha hivihivi Mtatiro, lazima nichukue hatua. Hawa niliwaalika kama marafiki tu, tukala wote chakula. Mbona hata kesho nimealikwa na Kajubi Mukajanga (Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania), hivi nikienda kukutana naye ndiyo atakuwa amenipa rushwa?”
Waziri mwingine ambaye jina lake linahifadhiwa kwa sababu hakupatikana kujibu tuhuma zake anadaiwa kuwaalika wawakilishi wa vyuo vya elimu ya juu, huku mbunge mmoja pia akidaiwa kuwaita wafugaji.
Kulikuwa na mgawanyiko wa wazi katika kanuni hiyo ya upigaji kura, CCM kikitaka kuungwa mkono kwa utaratibu wa kupiga kura za wazi huku wapinzani wakitaka za siri kama zilivyokuwa zimependekezwa na Kamati ya Kumshauri Mwenyekiti wa Muda kuhusu Kanuni.
Akizungumzia suala hilo, Mjumbe wa Bunge hilo, Makersia Jibubu alisema: “Sikutarajia haya. Nilichojua, tungefika wiki ya kwanza tukapitisha kanuni na baada ya hapo tukaendelea na mijadala. Lakini kinachoonekana ni mivutano ya wanasiasa na kibaya zaidi wote wanalenga kundi la wajumbe wateule wa Rais.”
Alisema alianza kuwa na wasiwasi kuhusu Bunge hilo, mara tu alipofika na kundi lake kuitwa na moja ya vyama vya siasa kufanya mazungumzo kwa lengo la kutaka ushawishi wao.
“Makundi yote yaliyoteuliwa na Rais yaliitwa na vyama vya siasa. Wakaandaa mikutano kwa chakula na vinywaji, halafu wakaanza kueleza sera zao. Nikasema sasa hii ni kwa faida ya nani?”
Mkutano wa CCM
CCM kilifanya mkutano wa wajumbe wake juzi usiku chini ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Ali Seif Idd. Pamoja na mambo mengine, kinadaiwa kutoa msimamo kuwalazimisha wajumbe wake kuunga mkono kura ya wazi.
Chama hicho kilitumia takriban muda wa saa tatu kuwafunda wajumbe hao ili kuhakikisha kuwa wanatetea utaratibu huo. Mkutano huo ulianza saa 2:15 hadi saa 5:00 usiku.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho, zilidokeza kuwa ajenda kuu ilikuwa ni kupitia rasimu ya kanuni.
Mjumbe mmoja alisema: “Inavyoonekana sasa suala la kupiga kura ya wazi ni amri na halina tena mjadala, lakini litaleta matatizo makubwa mbele ya safari… yetu macho.
“Mle ndani sisi wengine tuliamua kunyamaza kimya, maana hata unaposimama na kuchangia bado watu wanakuona kama ni msaliti.”Wakati wa semina ya wajumbe kuhusu rasimu ya kanuni, wajumbe wawili kutoka CCM, Ester Bulaya na Profesa Juma Kapuya waliweka wazi kuwa wanaunga mkono kura za siri, huku Anna Kilango akisema suala la ama kupigwa kura ya wazi au ya siri liamuliwe kwa kura ya siri kwa kuwa limezua mvutano.
Kikao cha Ukawa
Katika hatua nyingine, wapinzani na wajumbe wa makundi mengine ya kijamii chini ya Umoja wao wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), walikutana katika Ukumbi wa Pius Msekwa na kuweka msimamo wa kupinga kura ya wazi kwa nguvu na gharama zozote.
Mmoja wa wajumbe wake, John Mnyika alisema uamuzi mwafaka ni kura ya siri kuamua vifungu mbalimbali vilivyomo katika Rasimu ya Katiba. Mjumbe Tundu Lissu alisema: “Hatutakubali zipigwe kura za wazi, sisi bado tumesimamia palepale.”
Sitta na Suluhu wapitishwa
Habari zilizopatikana jana jioni zinasema wajumbe wa Bunge hilo wa CCM walikutana na kuwapitisha Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan kuwania nafasi za uenyekiti na makamu mwenyekiti’.