Stori: Imelda Mtema
SIKU chache baada ya mtangazaji Penniel Mungilwa ‘VJ Penny’ kupatana na Beutiful Onyinye, Wema Isaac Sepetu, mwigizaji Kajala Masanja ‘Kay’ naye ameibuka na kuweka bayana kuwa hata yeye yupo radhi na anatamani kupatana na Wema ambaye wameogelea kwenye bifu miezi kadhaa sasa.Kajala alifunguka hayo mara baada ya paparazi wetu kumuuliza kuhusiana na mtazamo wake juu ya Wema na Penny kupatana ndipo aliposema amefurahi mno na hata watu wengine watakuwa wamejifunza kitu kutokana na kupatana kwao.
Akizidi kushusha ‘vesi’ mbele ya kinasa sauti cha Risasi Jumamosi, Kajala alisema anaamini siku zote bifu zinarudisha nyuma maendeleo hivyo Wema kupatana na Penny ni jambo la busara kwani ni moja ya chachu ya kufanya mambo mengine yaendelee kwani hata yeye hapendezwi na mabifu.“Hata mimi natamani kupatana na Wema. Mabifu ni mambo ya kitoto sana, kwa kweli nimefurahi sana kuona Penny na Wema wamepatana kwani ni marafiki wa siku nyingi sana na wanastahili ifike sehemu vitu viishe na maisha yaendelee kama kawaida,” alisema Kajala.
Alipoulizwa Kajala kama kweli yupo tayari kupatana na Wema na uwezekano huo upo, Kajala alisema muda wowote wanaweza kukaa na kumaliza tofauti zao.“Hata mimi siku si nyingi tutaweka mambo sawa kwa sababu bifu hazijengi, hazina maana hata kidogo ni kufanya mambo yasiende mbele tu, inabidi tubadilike,” alisema Kajala.Wema na Kajala walikuwa mashosti wa damu lakini mwaka jana mwishoni waligombana huku chanzo kikitajwa kuwa ni kugombea mwanaume ambaye alifahamika kwa jina la CK.