Mkuu wa sera za mambo ya nchi wa umoja wa ulaya,Federica Mogherini
Mkuu wa sera za mambo ya nchi wa Umoja wa Ulaya, Federica Mogherini ametahadharisha kwamba tatizo la uhamiaji katika bahari ya Mediterranea ni kubwa na linahitaji utatuzi wa kipekee.
Akilihutubia baraza la usalama la umoja wa mataifa, Federica Mogherini amesema kipaumbele kwa bara la Ulaya sharti iwe ni kuokoa maisha katika eneo la bahari- lakini amesisitiza kwamba hakuna miujiza katika kupata utatuzi wa hilo. Amesema hakuna mhamiaji au mkimbizi atakae rudishwa bila ridhaa yake.

"lazima tukubaliane na ukweli kwamba kuna makundi ya kihalifu, mitandao ya kihalifu inayofanya kazi mipakani ikiwa na mtandao mzuri kabisa huku wakitengeza fedha nyingi ambazo zinatumika kuwafanya watu watumwa kutokana na matatizo yao. Wanawauzia watu matumaini lakini badala ya matumaini wanauawa watu. Lazima tukabiliane na hilo bila hivyo, itakuwa hatuishi kwa misingi ya utu wetu na hadhi yetu. Bila shaka, hii haina maana kwamba hatutaweza kukabiliana na tatizo la kuwatunza watu tuliowaokoa.")
Mapendekezo mapya ya kukabiliana na tatizo la uhamiaji yatawasilishwa siku ya Jumatano wiki hii na Tume ya Umoja wa Ulaya. Mapendekezo hayo yatajumuisha mipango ya kuwepo kiwango maalumu cha wahamiaji ambao watachukuliwa na nchi zote wanachama wa Umoja wa Ulaya.
Sera ya Uhamiaji ya tume hiyo itakayotangazwa katikati mwa juma pia itapendekeza kuwepo kwa hatua za kisheria zitakazowaruhusu wahamiaji kuingia barani ulaya ili waepukane na kwenda kwa wafanya biashara hara mu ya kusafirisha watu.