WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakishirikiana na Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, jana iliendesha bomoabomoa ya nyumba zilizojengwa bila kufuata taratibu za ujenzi katika Manispaa hiyo.
Ubomoaji huo unatarajiwa kugusa maeneo 12 ambayo yapo katika maeneo mbalimbali ya Manispaa hiyo ikiwemo Mwenge, Sinza, Kinondoni Biafra, Tegeta na Bunju. Gazeti hili lilitembelea maeneo mbalimbali yaliyopaswa kubomolewa na kukuta ubomoaji ukiendelea bila vurugu licha ya wananchi kulalamikia kutotendewa haki.
Akizungumzia ubomoaji huo, Mhandisi Mkuu wa Manispaa ya Kinondoni, Baraka Mkuya alisema umefuata taratibu na wamebomoa nyumba 14 katika eneo la Mwenge, iliyopo Sinza. Aliongeza kuwa ubomoaji huo utaendelea leo katika maeneo ya Tegeta, Mbezi Beach na Bunju.
Licha ya ubomoaji huo kwenda salama, wananchi wengi wamelalamika kuwa hawakupatiwa taarifa mapema na wengine wakidai kubomolewa nyumba zao usiku huku wakishindwa hata kuokoa mali zao.
Katika eneo la Mwenge ambapo nyumba za makazi ya watu pamoja na biashara zilibomolewa, wananchi hao walisema zilibomolewa saa tisa usiku wengine wakiwa hata hawajaamka.
Akizungumza na gazeti hili, mkazi wa eneo hilo ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini, alisema wakati ubomoaji huo ukiendelea alikuwa ndani baada ya kusikia kuanguka kwa kuta, aliamka na kutoka nje bila kuokoa chochote.
|
0 Comments