Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Leonard Paul
WAKAZI wanne wa jijini Tanga wamekufa papo hapo na wengine wawili kujeruhiwa kwa risasi na majambazi .
Majambazi hao waliokuwa na bunduki aina ya SMG , walivamia juzi duka kuu (supermarket) la mfanyabiashara Hamoud Ali lililopo Mtaa wa Swahili katika kata ya Central jijini Tanga .

Waliokufa katika tukio hilo ni Ahmed John, Vitus Manfred ambaye ni dereva wa gari la Mahakama ya Hakimu Mkazi Tanga, Athumani Seya pamoja na Ali Mpemba ambaye ni mfanyakazi kwenye duka hilo.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Leonard Paul tukio hilo ni la juzi saa 1.30 usiku.
‘’Wakati biashara inaendelea ndani ya hilo duka kuu , ghafla waliingia watu wengine zaidi kama wateja ambao baada ya muda mfupi walibadilika na kutoa silaha za moto”, alisema.
Aliongeza “Kitendo chao hicho kilienda sambamba na amri ya kuwataka watu wote waliokuwa humo dukani kulala chini ambapo inadaiwa walitii na kisha wakaamua kuwapiga risasi maeneo ya kichwani wateja wanne waliokuwemo.”
Kamanda alisema majambazi hao walipora Sh milioni 2.7 na kukimbilia kusikojulikana.