Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei
WATU 11 wanashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumbaka msichana mwenye umri wa miaka 21, kisha kumpiga picha za utupu za video na kuzisambaza kwenye mitandao ya kijamii kuonesha tendo hilo la ubakaji.
Kati ya hao, wawili wanashikiliwa kwa kubaka na kumpiga picha msichana huyo, wakati tisa wanatuhumiwa kusambaza picha hizo za utupu kwenye mitandao ya kijamii.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei alisema jana mjini hapa, kuwa watuhumiwa hao walifanya kitendo hicho Aprili 28, mwaka huu, saa 1 usiku katika nyumba ya kulala wageni yenye jina la Titii iliyopo Kata ya Dakawa, Wilaya ya Mvomero.
Wakati kamanda akitoa taarifa hiyo, vile vile Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu pia alitoa kauli ya serikali bungeni mjini Dodoma, kulaani kitendo hicho na akawataka watu wote wenye video hiyo kuacha kuisambaza kwa kuwa ni udhalilishaji kwa wanawake.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda Matei alisema msichana huyo (jina limehifadhiwa), aliitwa kwenye nyumba hiyo ya wageni na mwanamume aliyefahamika kwa jina la Zuberi Thabiti (30) mkazi wa Mbarali, mkoani Mbeya; ambaye alikuwa na mahusiano naye kimapenzi.
Alisema baada ya kuingia chumbani, alimkuta mwanamume mwingine aliyefahamika kwa jina la Iddy Adamu (32), mkazi wa Makambako.
Kamanda alisema mwanamume huyo, alimlazimisha msichana kufanya mapenzi huku akimrekodi picha za video na baadaye kuzisambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii. Kwa mujibu wa kamanda, watuhumiwa hao pia walimtishia kisu msichana huyo asipige kelele wakati akifanyiwa kitendo hicho na kumtaka asitoe siri hiyo vinginevyo watamuua.
Kamanda Matei alisema uchunguzi wa tukio hilo unaendelea wakati polisi ikiendelea kuwatafuta watuhumiwa wengine waliosambaza picha hizo za video wafikishwe mahakamani.
Aliendelea kuonya wananchi kwa kuwataka kuepuka kusambaza picha za ngono kwenye mitandao ya kijamii, vinginevyo sheria itachukua mkondo wake.
Serikali yalaani Awali, Waziri Ummy alilaani kitendo hicho kwa kutaka hatua stahili zichukuliwe dhidi ya watuhumiwa.
Alitoa kauli hiyo baada ya Mbunge wa Viti Maalumu, Kemilembe Lwota (CCM) kuomba mwongozo kwa Mwenyekiti wa Bunge, Musa Zungu kuhusu video hiyo inayosambazwa.
Mbunge huyo wa viti maalumu alisema ipo video inasambazwa katika mitandao ya kijamii, inayomdhalilisha msichana wa kitanzania akifanyiwa vitendo hivyo, ambavyo vinakiuka mila na desturi za Mtanzania.
Ummy alisema, akiwa waziri anayesimamia masuala ya wanawake na watoto pamoja na serikali, wanalaani kitendo hicho kilichofanywa cha kumdhalilisha mwanamke.
Alisema baada ya kuiona na kuwasiliana na Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Ernest Mangu, watuhumiwa hao wamekamatwa.
Alisema ana imani watafikishwa mahakamani mapema iwezekanavyo. Aliwataka wanaume kuheshimu wanawake wote huku akisisitiza kuwa suala hilo halivumiliwi.