Raia wa Afrika Mashariki waishio Zimbabwe wamekutana mjini Harare kuanzisha utaratibu wa ushirikiano kuanzia katika nchi zao na hata wawapo nje ya Afrika Mashariki.
Pamoja na kuwakutanisha kwa mara ya kwanza nchi zote za Afrika Mashariki pia wameitumia siku hii kumkaribisha mwanachama mpya Sudan ya Kusini.

"Sisi ni watoto,hatuwezi kula ugali na watu wazima, ninachukua nafasi hii kuomba mtulee tukue tuwafikie" amesema Gabriel Riek Balozi wa Sudan Kusini nchini Zimbabwe.
''Sudan Kusini ina fursa nyingi kwa nchi wanachama ikiwamo kuwakaribisha kufundisha Kiswahili kwani nchi hiyo imeanza kusisitiza lugha ya Afrika Mashariki'' aliongezea balozi Riek
Naye Balozi wa Kenya nchini Zimbabwe Bi Lucy Chelimo amesema ''Tumefurahishwa sana na siku ya leo kwani mara zote kila nchi imekuwa ikifanya matukio yake hali ambayo imekuwa inachelewesha mshikamano''
Aidha Balozi Chelimo ameahidi kuwa nchi zote wanachama ziko tayari kuisaidia Sudan Kusini kuimarika.
"Tutawalea, tena kwa maziwa..." Amesema balozi Chelimo
Image captionGabriel Riek Balozi wa Sudan Kusini nchini Zimbabwe.
Kwa upande wake balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe Charles Lawrence Makakala amesema kila mwaka watahakikisha wanawakutanisha wananchi wa Afrika Mashariki waishio hapa ili kufahamiana na hata kubadilishana taarifa zinazoweza kufungua fursa miongoni mwao.
Wananchi wa nchi zote sita zinazounda jumuiya ya Afrika mashariki waliofika katika tukio hili lililofanyika katika ubalozi wa zamani wa Tanzania mjini Harare wamesema wamejifunza mengi kwani kila mmoja kuna lililomleta Zimbabwe hivyo wamebadilishana ujuzi na pia watoto wao wameanza kufahamiana jambo ambalo litawaandaa kuiendeleza Afrika Mashariki siku za usoni.
Mwenyekiti wa watanzania waishio Zimbabwe Apatae Fatacky amesema wazo hili lilianzishwa na dada mmoja raia wa Rwanda, waliobakia wamelifanyia kazi.