Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa.
WIZARA ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imeomba kuidhinishwa Sh trilioni 4.8 kwa ajili ya mwaka ujao wa fedha ambazo kati ya hizo, sekta ya ujenzi imetengewa sehemu kubwa ya fedha zitakazojenga barabara ikiwemo kuondoa msongamano katika Jiji la Dar es Salaam.

Licha ya sekta ya ujenzi ambayo imetengewa Sh trilioni 2.1, kwa upande wa uchukuzi, miongoni mwa maeneo ambayo bajeti imeyapa kipaumbele, ni pamoja na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) lililotengewa Sh bilioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa ndege zaidi ya tatu.
Kwa upande wa reli, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, katika kuwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya wizara hiyo, alisema Sh bilioni 9.5 zimetengwa kwa ajili ya usanifu wa kina na kuanza ujenzi wa reli ya Standard Gauge.
Fedha za ndani Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi, Profesa Mbarawa alisema sekta ya ujenzi imetengewa Sh trilioni 2.2 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa fedha za ndani kutoka mfuko mkuu serikalini na mfuko wa barabara.
Alisema katika mfuko wa barabara, wanatarajia kukusanya Sh bilioni 832.3 zitakazotumika kufanya kazi za matengenezo ya barabara nchini. Alisema katika ujenzi wa barabara kuu, zimetengwa Sh bilioni 16.5 kwa kufanya upembuzi yakinifu kwa kilometa 3,184 .
Alisema Sh 29,773,307,730 watatumia kwa ajili ya barabara za mikoa kwa kutumia mfuko wa barabara kwa kukarabati kilometa 584.30 kwa kiwango cha changarawe na kilometa 36.9 kwa kiwango cha lami. Msongamano Dar Alisema katika kuondoa msongamano katika jiji la Dar es Salaam, Sh bilioni 38.9 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara za kilometa 111.85.
Alitaja barabara hizo kuwa ni mzunguko wa Kawawa-Msimbazi- Jangwani/ Makutano ya Twiga, Tabata Dampo-Kigogo, Kimara Kilungule-External na Mbezi Malambamawili- Kinyerezi- Banana. Pia alisema fedha hizo zitatengeneza barabara ya Tegeta–Wazo Hill- Goba-Mbezi, Goba-Mbezi Mwisho, Tangi Bovu-Goba, Kimara Baruti- Changanyikeni na kwingineko.
Barabara nyingine Alisema katika mwaka ujao wa fedha, Sh bilioni 30 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara za mikoa na madaraja katika mikoa yote nchini. Alisema kwa upande wa miradi ya barabara na madaraja itakayojumuisha ujenzi wa njia ya Express ya Dar es Salaam-Chalinze-Morogoro yenye kilometa 200 na Dar es Salaam -Chalinze kilometa 128, imetengewa Sh bilioni 12.6 kwa ajili ya upembuzi yakinifu pamoja na nyaraka za zabuni kwa ushirikiano na sekta binafsi.
Alisema katika ujenzi wa madaraja makubwa, katika mwaka huu wa fedha zimetengwa Sh bilioni 47.2 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa madaraja ya Kirumi (Mara), Sibiti (Singida) na Sukuma (Mwanza).
Madaraja mengine na mikoa yake kwenye mabano ni Kilombero (Morogoro), Kavuu (Katavi), Mbutu (Tabora), Momba (Songwe/Rukwa), Simiyu (Simiyu) Lukuledi II (Lindi) pamoja na daraja jipya la Wami (Pwani).
Waziri Mbarawa alisema wizara yake pia imetenga Sh bilioni 17.9 kwa ajili ya barabara ya Kyaka-Bukene mkoani Kagera, yenye kilometa 170. Mbarawa alisema kati ya barabara na madaraja hayo, jumla ya kilometa 712.40 zitajengwa kwa kiwango cha changarawe na kilometa 63.8 kwa kiwango cha lami pamoja na ujenzi wa madaraja 15. ATCL kufufuka?
Akizungumzia ununuzi wa ndege, Waziri Mbarawa alisema fedha hizo; Sh bilioni 500 zitanunua ndege zisizopungua tatu. Hata hivyo, alisema idadi kamili ya ndege zitakazonunuliwa na bei ya kila ndege itajulikana baada ya uchambuzi wa suala hilo kukamilika. Vilevile alisema wametenga Sh bilioni 200 kwa ajili ya utekelezaji miradi mbalimbali katika Mamlaka ya Viwanja vya Ndege.
Reli, bandari Alisema serikali inatarajia kuwasilisha bungeni sheria mpya ya Tazara kuboresha utendaji wake. Vilevile alisema, watakamilisha usanifu wa kina wa njia ya reli kati ya Tanga-Arusha na upembuzi yakinifu wa usanifu wa awali wa ujenzi wa reli hiyo ya standard gage.
Alisema reli ya Arusha-Musoma pamoja matawi yake kwenda Engaruka na Minjingu, zimetengewa Sh bilioni 9.7. Akizungumzia ujenzi na upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, alisema wametenga Sh bilioni 342 kuimarisha na kuongeza kina cha gati namba 1 hadi 7, kujenga gati jipya na kukamilisha jengo la huduma kwa wateja.
Kuhusu Shirika la ReliTanzania (TRL), alisema mwaka huu wa fedha wamepanga kusafirisha tani 537,500 za mizigo na abiria 541,000 na wakati huo huo kuendelea kukarabati mabehewa ya abiria na mizigo.
Mawasiliano, TTCL Kwa upande wa sekta ya mawasiliano, Waziri Mbarawa alisema Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) inatarajia kuongeza idadi ya wateja wa huduma mbalimbali za simu kutoka 74,790 wa mwaka jana hadi 815,000 ifikapo mwaka 2018. Pia wanatarajia kuanzisha na kuendesha mtandao wa kisasa wa simu za kiganjani na kuboresha mtandao wa data na simu za waya au mezani ili kuleta ufanisi kwa wateja.