Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga amesema serikali haifichi mkataba wowote ukiwamo wa Lugumi Enterprises, isipokuwa wabunge wanapaswa kufuata taratibu ili kuona mikataba hiyo kama kanuni zinavyowaelekeza.
Kitwanga alisema hayo juzi usiku bungeni wakati akifanya majumuisho ya mjadala wa hotuba yake ya bajeti kwa mwaka wa fedha 2016/17. Kuliibuka mjadala mzito kuhusu masuala ya mikataba ukiwamo wa Lugumi na Jeshi la Polisi, kiasi cha kuwa moja ya sababu za wabunge wa upinzani kukataa kusoma maoni yao kuhusu hotuba hiyo ya Waziri Kitwanga.

Kitwanga alipojibu hoja za wabunge, alisema hakuna anayeficha mikataba yoyote katika wizara hiyo kwani hata hiyo mikataba inayozungumzwa aliiwasilisha katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama alipotakiwa kufanya hivyo.
“Hata huu mkataba wa Lugumi unaweza kuonwa na mbunge yeyote ila kuna taratibu zake. Pia wabunge msisahau haya ni masuala ya usalama, yanaiweka nchi katika hali ya utata,” alisema Kitwanga. Aliendelea, “Mkataba upo na uko wazi, lakini hizi kelele za magazeti zinaiweka nchi katika hatari.
Hakuna anayeficha kitu, lakini tufuate taratibu zilizowekwa. Tunapiga kelele sana. Tunalo (wabunge) jukumu la kulinda usalama. Tufuate taratibu zilizo sahihi kuomba taarifa tunazohitaji.” Kitwanga alisema amesikitishwa na maneno yaliyowekwa katika maoni ya Kambi ya Upinzani ambayo yalitakiwa kufanyiwa marekebisho kabla ya kusomwa bungeni juzi asubuhi.
“Baada ya kusoma bajeti mbadala nimesikitika sana. Bila CCM nchi hii haina serikali mbadala. Yaani hotuba nzima imejaa rejea ya magazeti. Kambi ya Upinzani iliyopo ni kambi ya upingaji,” alisema Waziri Kitwanga.
Alisema badala ya wapinzani kujikita katika rejea ya magazeti na maneno ya kusikia, alitarajia waseme kile wanachowaza wao. “Niko serikalini kwa miaka 35 sasa. Natambulika kama Mr STK, Mzee wa STK – Sheria, Taratibu na Kanuni.
Nimewasilisha fomu yangu Sekretarieti ya Maadili kwa mara ya kwanza mwaka 1998. “Hivyo vinatosha kuwapa taarifa mimi ni mtu wa aina gani, sipendi kusema, napenda kutenda,” alisema Kitwanga ambaye ni Mbunge wa Misungwi mkoani Mwanza.
Akijibu hoja nyingine, alisema uhakiki wa madeni ya Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) unaendelea. Alisema zipo taasisi tatu za umma; Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) na Mamlaka ya Ununuzi wa Umma (PPRA) zinafanyia kazi masuala mbalimbali ndani ya Nida.
Alisema Sh bilioni 50 zipo Hazina na ziko tayari kulipa wafanyakazi ambao waliamuriwa kuachishwa kazi. Hata hivyo alisema, hilo litafanyika kwa uhakiki ili kutolipa wafanyakazi hewa.
Alikiri kuwa askari hawana makazi mazuri na bado maslahi yao ni ya kiwango cha chini. Alisema serikali inayafanyia kazi ikiwamo ujenzi wa nyumba za kuishi pamoja na kuongeza mishahara yao.
Akijibu hoja za wabunge kuhusu kuongezwa fedha kwa Nida ili ikamilishe kazi zake mwishoni mwa mwaka huu, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango, alisema fedha zilizotengwa kwa mamlaka hiyo katika bajeti zinatolewa ili kazi zifanyike.