Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwezeshaji, Charles Mwijage
HALI ya upatikanaji sukari nchini, imeanza kuwa kwenye mwelekeo mzuri, baada ya tani zaidi ya 10,000 kuingizwa kutoka nje. Nyingine 31,000 zinasubiriwa kuwasili huku viwanda vya bidhaa hiyo pia vikianza uzalishaji wiki hii.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage alitoa taarifa hiyo jana bungeni wakati mjadala wa bajeti ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ukihitimishwa.
Akielezea sukari inayoingia kutoka nje, Mwijage aliwataka wafanyabiashara wote wanaojishughulisha na bidhaa hiyo, kujitambulisha kwa wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya ili wanayopewa Dar es Salaam, waifikishe kwa viongozi hao waione.
Kuhusu viwanda ambavyo awali vilitarajiwa kuanza uzalishaji Julai mwaka huu, Mwijage alisema, “Adha ya sukari iliyokuwepo, sasa inakwenda kuisha. Kuna sukari ya kutosha…kwani leo kiwanda cha Kagera Sugar kimeanza kuzalisha tani 250.”
Waziri Mwijage alisema pia Kiwanda cha Kilombero (K One), kimeanza kuzalisha na kitazalisha tani 600 kwa siku. Wakati matumizi ya nchi ni tani 1,200 za sukari kwa siku, Mwijage alisema tofauti iliyobaki ndiyo imeagizwa kutoka nje.
Aliwataka wabunge kutambua kuwa uamuzi uliochukuliwa na serikali, ulijenga imani na kuleta wawekezaji. Alisema hivi sasa, Kiwanda cha Sukari Kagera kinapanua eneo la Kitegule na kuzalisha tani nyingine 60,000 na pia kukiwa na mwekezaji kutoka Oman, ambaye ataongeza uzalishaji katika kiwanda hicho na kufikia tani 300,000.
Alisema adha ya sukari ambayo nchi inapitia sasa ni kwa ajili ya kudhibiti uingizaji sukari na kisha kuleta wawekezaji kwenye uzalishaji wa sukari. Mwijage alisema hali ya sukari ni ya kutosha na sasa wamechukua hatua ya kujenga kiwanda cha Kigoma Sugar katika eneo la hekta 47,000.