Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk Leonard Akwilapo
SHULE zote ambazo hazijasajiliwa zimepewa miezi miwili ziwe zimesajiliwa, kabla ya serikali kuzifunga baada ya muda huo kuisha.
Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk Leonard Akwilapo alisema hayo jana.

Kwamba ifikapo Julai 30 mwaka huu, mmiliki wa shule itakayobainika kutosajiliwa, ikiwemo zitakazokosa vigezo vya kusajiliwa, atapaswa kuhamisha wanafunzi waliopo kwa gharama zake.
Alisisitiza wahusika wasajili shule hizo kabla ya tarehe hiyo. Alisema kuwa agizo hilo ni kutekeleza Sheria ya Elimu Sura ya 353, inayoelekeza shule zote kusajiliwa kabla ya kusajili wanafunzi.
Akwilapo alisema kwa kutofuata utaratibu huo wa kusajili shule, wanafunzi wanaotoka katika shule au vituo hivyo hufanya mitihani ya taifa, ikiwemo mtihani wa maarifa (QT) na mitihani mingine ya taifa (Kidato cha Nne na Sita) kama watahiniwa wa kujitegemea.
Alisema pia baadhi ya wanafunzi hao huingizwa kwa utaratibu usio rasmi, kufanya mitihani ya Darasa la Nne na Darasa la Saba katika shule zilizosajiliwa bila kuzingatia mazingira ya mahali waliposomea, hali inayochangia kwa kiasi kikubwa kushindwa katika mitihani hiyo.
“Wamiliki wote wa shule ambazo hazijasajiliwa wanatakiwa kuwasilisha maombi yao katika Ofisi za Uthibiti Ubora wa shule Kanda, Wilaya au Idara ya Ithibati ya shule (Usajili) Makao Makuu ya wizara kabla au ifikapo Julai 30 mwaka huu,” alisema.
Alipoulizwa ni shule ngapi ambazo zinajiendesha bila kusajiliwa, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ithabati ya Shule, Khadija Mcheka alisema: “Hapa nilipo sitaweza kukupa takwimu sahihi, lakini kwa mkoa wa Dar es Salaam tumeshafungia shule za awali na msingi zipatazo 23.” “Tatizo kubwa lipo kwenye shule za awali na msingi ndio nyingi ambazo zinatoa huduma ya elimu bila kusajiliwa, kwa shule za sekondari ni kidogo,” alisema.