Sehemu ya jumba kubwa la kibiashara mjini Mombasa imeporomoka siku chache baada ya jumba la makazi kuporomoka jijini Nairobi na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 40.
Sehemu ya jumba hilo la Nyali Centre, yenye ghorofa sita, iliporomoka usiku wa kuamkia Jumatatu.

Hakuna aliyeripotiwa kujeruhiwa wakati wa mkasa huo.
Jumba la Nyali Centre huwa na kituo cha mazoezi na mgahawa maarufu.
Waziri wa serikali ya jimbo la Mombasa Francis Thoya amesema jumba hilo litachunguzwa kubaini iwapo ni thabiti.
“Nadhani sehemu ambapo vyoo hivyo vilifaa kuuunganishwa na jumba lenyewe ndiyo ilikuwa na shida. Ninamsaka mhandisi na aliyepewa kandarasi,” amesema.
“Lakini unapopata visa kama hivi, ni ishara tosha kuwa inafaa tuchunguze upya mijengo yetu. Kwa hivyo kutakuwa na ukaguzi wa baadhi ya mijengo mikuu ambayo inatumiwa na umma.”