Serikali ya Tanzania imeagiza sukari ilikukabiliana na upungufu wa sukari uliopo nchini.
Rais wa Tanzania Joseph Pombe Magufuli amesema badala ya kuwapa wafanyabiashara leseni ya kuagiza sukari kutoka ng'ambo serikali yenyewe ndio itaagiza sukari hiyo moja kwa moja.

Kauli hiyo inawadia baada ya mabohari zaidi kugunduliwa kote nchini yakiwa yamejaa sukari iliyoagizwa kutoka nje na ile iliyonunuliwa kwa wingi kutoka kwenye kampuni za kusaga sukari za humohumo Tanzania.
''Kuna mmoja ambaye amepatikana Arusha amehodhi zaidi ya tani elfu tano ya sukari naye mwengine huko Kilombero amenunua sukari yote kutoka kwa kampuni za humu humu nchini na akaficha.''
''Lakini hili ni swala la sasa tu, katika siku zijazo sukari itapatikana kwa wingi hapa Tanzania.Serikali imekwisha agiza sukari lakini hatutawapa hawa waliofilisi watanzania leseni ya kuingiza tena sukari.
''Serikali imeagiza na itauza sukari hiyo kwa bei ya chini,,,, hiyo ndio lengo la serikali '' alisema rais Magufuli huku mawananchi wakimshangilia.
Image caption''Katika siku zijazo sukari itapatikana kwa wingi hapa Tanzania.Serikali imekwisha agiza sukari lakini hatutawapa hawa waliofilisi watanzania leseni ya kuingiza tena sukari.''
Sukari hiyo ambayo huwa ni ya bei ya chini hubadilishwa na kisha kuvikwa magunia ya makampuni ya Kitanzania yanayosaga sukari na kisha kuuzwa rejareja.
Tumbua tumbua ya rais Magufuli imesadifiana na tangazo la Halmashauri ya ushuru ya Tanzania TRA kuwa imeanza kugawa sukari iliyoingizwa nchini kinyume cha sheria na kufichwa katika mabohari kote nchini.
TRA ilichukua hatua hiyo baada ya mwekezaji wa kibinafsi mkoani Lindi kupatikana na zaidi ya mifuko elfu tano za sukari kutoka nga'mbo.
Yamkini sukari hiyo hubadilishwa kwenye mifuko yenye nembo ya kampuni za kusaga sukari za Tanzania na kisha kuuzwa kwa bei maradufu.