Mwanamume mmoja katika mji wa Bungoma, Magharibi mwa Kenya ameshangaza wengi baada ya kudandia helikopta ambayo imepaa na kuondoka naye.
Helikopta hiyo ilikuwa imesafirisha mwili wa mfanyabiashara mashuhuri Jacob Juma aliyeuawa kwa kupigwa risasi jijini Nairobi wiki iliyopita, vyombo vya habari nchini Kenya vinasema.

Video zinazosambaa mtandaoni zinaonesha helikopta hiyo ikipaa juu angani kutoka uwanja wa Posta, mwanamume huyo akiwa amejishikilia kwenye vyuma vya helikopta hiyo.
Taarifa zinasema baadaye ndege imetua kwa dharura katika uwanja wa ndege wa Bungoma na mwanamume huyo akapelekwa hospitalini.
Kitambulisha mada #Bungoma kimeanza kuvuma kwenye Twitter nchini Kenya, watu wakijadili tukio hilo.
Wengi wameeleza kushangazwa kwao na wengine wanalifanyia mzaha.
Baadhi wanasema mwanamume huyo alisahau leo ilikuwa Ijumaa tarehe 13, ambayo kwa baadhi ni siku yenye kutokea mabaya.
Wengine wanatumia majina ya filamu na hata nyimbo. Mfano wimbo wa 'I Believe I Can Fly', wake R Kelly na filamu ya Mission: Impossible ambayo mwigizaji nyota wake ni Tom Cruise.