Rais Dkt. John Pombe Magufuli amewaonya wanaoficha Sukari na kutishia kuichukua Sukari hiyo na kuigawa bure kwa wananchi. Rais Magufuli ametoa onyo kali kwa wafanyabiashara walioficha sukari ili baadae waiuze kwa bei ya juu.
Amesema wafanyabiashara hao wenye tamaa ya pesa walikuwa wakifuata sukari iliyo Expire huko Brazili na kuileta nchini ili watengeneze faida na ndo maana serikali iliwapiga marufuku kuagiza.

Rais Magufuli ameyasema hayo leo wakati akiwasalimia wananchi wa Katesh, Mkoani Manyara. Rais ametoka Mkoani Dodoma leo, anaelekea Mkoani Arusha kwa usafiri wa gari.
Akiongea na mamia ya wananchi hao waliojitokeza kumlaki njiani, Rais Magufuli amewatoa hofu wananchi kuhusu uhaba wa sukari kwa kuwa tayari wako katika mchakato wa kuagiza makontena ya sukari nje ya nchi ili kuwakabili wafanyabiashara walioficha bidhaa hiyo.
Amesema kwa taarifa alizonazo, kuna mfanyabiashara alienda akanunua sukari pale Kilombero zaidi ya Tani 3000 na hataki kuzichukua hadi leo.
Pia amesema kuna mwingine ana godauni Mbagala yenye Tani 4000 ambazo hataki kuzitoa ili wananchi wakose sukari.
Rais Magufuli amesema ameviagiza vyombo vya dola viwafuatilie ili ikithibitika sukari waliificha, basi ichukuliwe na kugawiwa bure kwa wananchi na pia watapigwa marufuku kufanya biashara yoyote hapa nchini.