Mgombea Urais wa Republican anaonekana kulegeza msimamo kuhusiana na pendekezo lake tata la kuwazuia Waislamu kuingia Marekani.
Katika mahojiano na kituo cha television cha Fox News, Donald Trump akijibu kauli ya meya mpya wa mji wa London Sadiq Khan, ambaye awali alionyesha wasiwasi na kusema hataweza kuingia nchini Marekani chini ya utawala wa Donald Trump, Trump ameiambia Fox News kwamba meya huyo anaweza kuja kwani hayo yalikuwa ni maoni tu.

Hata hivyo, Bwana Khan amekataa ukarimu huo wa Trump ambao unamlenga yeye pekee na sio kwa ajili ya jamii yote ya waislamu.
Pendekezo la kuwazuia waislamu kuingia nchini Marekani lilipata upinzani mkubwa ndani na nje ya Marekani.
Wakati huo huo, Waziri mkuu wa Uingereza, David Cameron, ameomba msamaha kwa kiongozi wa dini ya kiislamu baada ya kumtaja kuwa ni mfuasi wa kundi la Islamic State.
Cameron alitoa kauli hiyo bungeni wiki tatu zilizopita katika kampeni za kutafuta meya mpya wa London. Bwana Cameron amesema mgombea wa upinzani Sadiq Khan - ni muislamu aliyeshinda kiti hicho cha umeya, ameonekana mara kadhaa na iman Sulaiman Ghani, imamu mstaafu.
Kwa upande wake, Iman Ghani ametishia kuchukua hatua za kisheria kutokana na madai hayo kwamba yeye ni mfuasi wa Islamic State.