Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema aina ya virusi vya Zika ambavyo vimekuwa vikisababisha watoto kuzaliwa na vichwa vidogo vimegunduliwa Afrika kwa mara ya kwanza.
Virusi hivyo vimesababisha taharuki nchi za Amerika Kusini, na hasa Brazil.

Virusi hivyo vilipatikana katika visiwa vya Cape Verde.
Jina la virusi hivyo linatokana na msitu wa Zika, Uganda ambapo virusi hivyo vilitambuliwa kwa mara ya kwanza 1947.
Lakini aina ya virusi hivyo ambayo imekuwa ikipatikana Afrika haikuwa hatari zaidi na ilisababisha dalili za mafua ya kawaida.
Wengi wa wanaoambukizwa aina ya awali ya virusi walikuwa wakipatwa na homa ambayo si kali sana, mwasho na maumivu katika maungio.
Mlipuko wa sasa ulianza mwishoni mwa mwaka 2015 nchini Brazil na dalili zake zimekuwa kali.
Virusi vya Zika huenezwa sana na mbu ingawa kumeripotiwa pia visa vya watu kuambukizwa virusi hivyo kupitia kufanya mapenzi.