Wanafunzi wa darasa la kwanza katika shule za msingi, 151, nchini Kenya wamepokea kompyuta hizo siku ya Jumanne.
Usambazaji wa tablets hizo unahusisha wanafunzi 11,570 wa darasa la kwanza katika shule 151 zilizoteuliwa.

Katika kaunti ya Mombasa, wanafunzi wa shule ya Upili ya Sparki wamekabidhiwa kompyuta hizo.
"Tumepokea 'tablets' 80, laptopu mbili zitakazotumiwa na walimu pamoja na mashine moja ya kifaa cha kuonyesha picha kwenye ukuta kwa kutumia mwanga". Anasema mwalimu mkuu wa shule ya msingi ya Sparki Alfred Nthiga.
Mwandishi wa BBC mjini Mombasa aliyeshuhudia utoaji wa vifaa hivyo anasema vimewekwa masomo ya sayansi, hisabati, kiingereza na Kiswahili kwa wanafunzi wa darasa la kwanza.
'Tablets' hizo zinawawezesha kutafuta maelezo kwenye mtandao wa 'google'.
Katika mkondo wa kwanza wa kutekeleza mradi huo, takriban shule tatu katika kila kaunti, wanafunzi watopokea 'tablets', huku walimu wakikabidhiwa laptopu
Kila shule iliyoteuliwa kupata vifaa hivyo kote nchini itawezeshwa kupata huduma za mitandao kwa kutumia Wi-Fi.
Mradi huo utaigharimu serikali ya Kenya dola milioni 170.
Mradi huo wa kuwapa wanafunzi wa darasa la kwanza tarakilishi bila malipo ni miongoni mwa ahadi kuu za uchaguzi ambazo serikali tawala ya Jubilee ilitoa mwaka wa 2013.
Image captionwanafunzi wapokea kompyuta Kenya
Hata hivyo utekelezwaji wa mradi huu umekwazwa na tetesi za ufisadi pamoja na kesi nyingi mahakamani.
Ahadi ya serikali ya Jubilee ya kutoa laptopu kwa kila mwanafunzi wa darasa la kwanza katika siku 100 za kwanza haikutimizwa na badala yake, laptopu zikabadilishwa na vibao vya 'tablets'
Serikali ya Jubilee pia iliahidi kuwapa wanafunzi wa shule za msingi maziwa bila malipo, ahadi ambayo hadi sasa haijatimizwa.
Baadhi ya wakosoaji wanashikilia kuwa mradi huo haufai kupewa kipau mbele ikizingatiwa matatizo chungu nzima yanayoikumba sekta ya elimu; ikiwemo migomo ya walimu wakidai nyongeza ya mishahara na ukosefu wa nguvu za umeme katika maeneo mengi ya mashinani nchini Kenya.