Vyama vya upinzani nchini Tanzania vimelaani hatua ya polisi nchini humo kupiga marufuku mikutano ya hadhara.
Jana polisi waliwatawanya wafuasi wa vyama vya upinzani mjini Kahama, Magharibi Kaskazini mwa Tanzania, ambapo walikuwa wamekusanyika muda mfupi kabla ya mkutano wa hadhara uliokuwa umeandaliwa na chama cha
Chadema Chadema walikuwa wazindue msururu wa mikutano ya hadhara nchi nzima waliyoiitwa "Operesheni Okoa Demokrasia" ambayo pamoja na mambo mengine ilikuwa inalenga kuishitaki serikali ya Rais John Magufuli kwa umma juu ya maswala kama vile kufungiwa kwa kurushwa moja kwa moja kwa vikao vya bunge na aina ya uongozi wa serikali ya Rais Magufuli
Hata hivyo polisi wamesema kutokana na sababu za kiusalama, hawataruhusu mikutano hiyo iendelee kufanyika.
Wameongeza pia kwamba mikutano hiyo ilikuwa inalenga kuwashawishi wananchi kuvunja sheria.Hata hivyo mwenyekiti wa Chadema taifa Freeman Mbowe amenukuliwa na vyombo vya habari akilaani marufuku hii ya polisi na kusema haikuwa ya haki.
"Hizi ni siasa za kibabe na kidikteta ambazo Rais Magufuli ameanza kuzionyesha kwanza kwa kuzuia bunge lisionekane moja kwa moja na sasa wanazuia mikutano ya hadhara" amenukuliwa bw Mbowe na gazeti moja la kila siku nchini Tanzania.