Uhusiano kati ya Marekani na Tanzania unaonesha dalili za kuimarika licha ya nchi hiyo kukatiza msaada wa awamu ya pili ya mradi wa changamoto za milenia (MCC-2) kwa Tanzania.
Balozi wa Marekani nchini Tanzania Mheshimiwa Mark Childress amesema hayo baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.

Bwana Childress alisema kuwa hivi karibuni ''kupitia shirika la misaada la Marekani, USAID tunatarajia kutia saini mkataba wa zaidi ya dola milioni 400 kwa ajili ya mwaka ujao.
''Aidha tumezungumza kuwa kutakuwa na dola milioni 800 zitakazotolewa na Marekani kwa ajili ya miradi mbalimbali na hii haihusiani na MCC.'' Alisema balozi Childress
"Ukweli ni kwamba tunayo mengi ya kufanya pamoja katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, elimu na kilimo na tutafanya kila juhudi kuhakikisha yanafanikiwa"
Rais Magufuli kwa upande wake alisema kuwa serikali yake itaendeleza kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano na Marekani.
Image captionMataifa kadha ya magharibi yaliahirisha misaada kufuatia mchakato wa uchaguzi wa Zanzibar
Aidha rais huyo alisema kwamba fedha za msaada kutoka Marekani ni muhimu kwa maendeleo ya Tanzania.
"Amekuja kutuhakikishia kwamba watatoa hela kwa ajili ya Tanzania na anasema sasa hivi watatoa zaidi ya dola milioni 800, na mkataba mwingine tunaweza tukasaini hata kesho wa dola milioni 410.
Rais Magufuli alisema ''Balozi anasema kutotoa hela za MCC hakuna maana kupotea kwa urafiki wa Tanzania na Marekani, urafiki wa Tanzania na Marekani upo pale pale na sasa wanaongeza hela nyingi zaidi katika kuonesha kwamba juhudi za ''Hapa kazi tu'' zinaendelea" Taarifa hiyo ya ikulu ilielezea.