Rais wa Marekani Barack Obama ametangaza kumuunga mkono Hillary Clinton kuwa mgombea urais wa chama cha Democratic katika uchaguzi mkuu utakaofanyika baadaye mwaka huu nchini Marekani.

Amechukua hatua hiyo muda mfupi baada ya kukutana na seneta wa Vermont Bernie Sanders ambaye amekuwa akikabiliana na Bi Clinton katika kinyang’anyiro cha kumchagua mgombea wa chama hicho.
Akizungumza kwenye video ambayo imepakiwa kwenye Twitter na Bi Clinton, Bw Obama amesema mgombea huyo ndiye aliyewahi kuhitimu zaidi kuwa rais wa Marekani.
“Niko pamoja naye, nina msisimko na nasubiri sana kutoka huko nje na kufanya kampeni na Hillary,” amesema Obama.

ObamaImage copyrightREUTERS
Image captionObama alikutana na Sanders ikulu ya White House

Wawili hao sasa wanatarajiwa kuanza kufanya kampeni pamoja.
Bw Sanders naye amesema yuko tayari kufanya kazi na mpinzani wake, Bi Clinton, kumshinda mgombea wa chama cha Republican Donald Trump katika uchaguzi mkuu.
Hata hivyo hakujiondoa kinyang’anyironi. Alisema ataendelea kufanya kampeni yake na kwamba anatumai atakutana na Bi Clinton hivi karibuni.