Rais wa zamani wa Marekani Bill Clinton amemsifu sana mkewe Hillary na kusema anafaa kuongoza taifa hilo.
Ameambia kongamano kuu la chama cha Democratic mjini Philadelphia kwamba mkewe ndiye “mfumaji bora zaidi niliyewahi kukutana naye”.
Kwenye hotuba yenye hisia kali, amemweleza Hillary kama “rafiki mkubwa” na akasimulia walivyokutana na jinsi anavyojitolea katika utumishi wa umma.
Saa chache awali, mkewe aliibuka kuwa mwanamke wa kwanza nchini Marekani kuidhinishwa kuwania urais na chama kikubwa
Bi Clinton alihitimisha shughuli za usiku huo wa Jumanne kwa ujumbe wa video ambapo alisema: “Siamini kwamba tumefanikiwa kuweka ufa mkubwa zaidi katika dari hili la kioo”, akirejelea hotuba ya mkewe Rais Barack Obama, Michelle, siku ya kwanza ya kongamano.
“Na iwapo kuna wasichana wadogo huko ambao hawajalala na wananitazama, ningependa kuwaambia, huenda nikawa rais wa kwanza mwanamke Marekani na mmoja wenu anaweza kunifuata.”
Awali, Bi Clinton alisimulia walivyokutana katika Chuo cha Uanasheria Yale mwaka 1971.
“Nilimuoa rafiki yangu mkubwa,” amesema. “Tumekuwa tukitembea na kuzungumza na kucheka pamoja tangu wakati huo.”

ClintonImage copyrightAFP
Image captionBi Clinton amewataka wasichana wawe na matumaini

Bi Clinton alipitisha wajumbe 2,382 wanaohitajika kutawazwa mgombea baada ya jimbo la South Dakota kutangaza matokeo yake.
Katika juhudi za kuashiria umoja katika chama, mpinzani wake wakati wa mchujo, Seneta wa Vermont Bernie Sanders alichukua maikrofoni na kumtangaza Bi Clinton kuwa mgombea mteule kwa kauli moja, tangazo lililokaribishwa kwa shangwe.
Awali, wakati wa hotuba yake rasmi Jumatatu, Bw Sanders alikuwa ametangaza: "Hillary Clinton lazima awe rais ajaye wa Marekani.”
Tangazo la Bw Sanders ni kama marudio ya kongamano la 2008 ambapo Bi Clinton alimtangaza Bw Obama kuwa mgombea mteule.
Bi Clinton atakabiliana na mgombea wa Republican Donald Trump katika uchaguzi mkuu Novemba.
Kura za maoni zinaonesha wawili hao wanakaribiana sana kwa uuungwaji mkono wa wapiga kura.