Shule nane za Sekondari nchini Kenya zimeteketea kwa moto usiku wa kuamkia leo katika maeneo tofauti nchini humo.
Inakadiriwa kuwa mali zenye thamani ya mamilioni ya shilingi ya Kenya zimeharibiwa na moto huo, huku mamia ya wanafunzi wakikosa mahala pa kulala.

Mabweni ndio yaliyochomwa moto hali iliyosababisha wanafunzi kupoteza mali zao kama vile vitabu na nguo zao ikiwemo za shule.
Matukio ya shule kuungua moto yamekuwa yakiongezeka katika siku za hivi karibuni nchini humo.
Mapema wiki hii wanafunzi 42 walipandishwa kizimbani nchini Kenya, katika mahakama tofauti kwa tuhuma za kuhusika na uchomaji moto shule.
Wengi wao wameachiwa kwa dhamana huku wakifanyiwa uchunguzi wa umri kuona ni nani ana umri wa kuweza kushtakiwa kama mtu mzima ama kushtakiwa kama mtoto.
Serikali ya Kenya imesema itawachukulia hatua kali wale wote watakao bainika kuhusika na matukio hayo.