Jaji mmoja wa mahakama ya juu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo amekiri kuwa alishinikizwa na majasusi na wakuu wake katika idara ya mahakama kumpata na hatia kiongozi wa upinzani Moise Katumbi.

Jaji Chantal Ramazani alikuwa miongoni mwa jopo la majaji waliokuwa wakisikiza kesi hiyo dhidi ya katumbi ambaye hakuwa mahakamani.
Jopo hilo la majaji lilimpata Katumbi na hatia na kumhukumu kifungo cha miaka mitatu gerezani kwa kuuza mali kinyume cha sheria.
Bi Ramazani, sasa hivi yuko mafichoni.
Anaamini kuwa kauli hiyo ya mahakama ilikusudia kumzuia kiongozi huyo wa upinzani katika kinyang'anyiro cha kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Uchaguzi mkuu nchini humo umepangwa kufanyika mwezi Novemba.
Haikuwezekana kupata maoni ya viongozi wake mkuu wa idara ya mahakama wala idara ya ujasusi nchini humo kuhusiana na madai ya jaji huyo.
Bwana Katumbi kwa upande wake anasema kuwa anakusudia kurejea nyumbani DRC mwishoni mwa juma.