Nalazimika kuyaandika haya baada ya jana kusikia mteja mmoja akimlalamikia fundi wake wa nguo (fundi cherehani japo kiuhalisia yeye ni mshonaji wa ngu), kutokana na fundi huyo kutokamilisha ushonaji wa nguo yake ambayo alitarajia kuivaa kwenye shughuli (Send Off) kwa wakati.


Baada ya kulalamika sana, aliishia kusema "yaani mafundi cherehani wote, mwalimu wao ni mmoja". Baada ya hapo aliketi katika kiti ili fundi akamilishe kazi aliyopewa ambapo muda huo sasa fundi nae kwa papara alikuwa akiendelea na ushonaji wa nguo hiyo ya mteja wake. Lakini si kweli kwamba mafundi cherehani wote mwalimu wao ni mmoja wala si kweli kwamba wote ni waongo hata kama wengi wao wako hivyo.

Lakini moyoni nikajiuliza, "hawa mafundi cherehani nani kawaroga? Kwa nini siyo waaminifu kwa wateja wao?" Nikagundua kwamba, wengi wao wametawaliwa na tamaa. Tamaa ya kupata tesa. Wanapokea kazi nyingi kiasi kwamba hadi wanashindwa kuzikamilisha kwa wakati.

Nikasema hapana, wengi wao ni wasomaji wa BMG, hebu ngoja niwashauri kidogo leo kwamba; mafundi cherehani umefika wakati sasa wa kubadilika. Waiepuke tamaa na wapokee kazi kulingana na uwezo wao wa kukamilisha kazi za wateja wao. 

Mfano, ikiwa unajua huna nafasi ya kukamilisha ushonaji wa nguo ya mteja ndani ya siku tatu, mwambie ukweli ili mteja achague kuacha kazi kwako kwa siku utakazompangia ama la, haina haja ya kuchukua kazi ya mteja, huku ukiwa na kazi nyingi zaidi. Mbaya zaidi kama ni kitambaa au kitenge unakikata na kukiweka kando. Kwa ushindani wa sasa, mtawapoteza wateja wengi na hiyo kazi mtaikimbia.

Pia wateja nao umefika wakati wa kuacha kulalamika. Zipo sehemu ambazo mafundi cherehani hawafanyi kazi kienyeji kama ilivyokuwa zamani. Wanafanya kazi kwa uadilifu na ukweli wa hali ya juu ili kurejesha imani kwa wateja wao. Imani ambayo imepotea kwa wateja walio wengi.

Mfano "Mikaela Professional Tailors" ambao ni wabunifu na washonaji wa nguo za aina mbalimbali Jijini Mwanza, sifa yao kubwa ambayo imewajengea imani tena kwa muda mfupi ni kukamilisha kazi za wateja wao kwa wakati. Pia uwekezaji wao ikiwemo mashine nyingi na za kisasa, unawafanya kukamilisha kazi za wateja, kuendana na kasi ya upokeaji wa kazi hizo.

"Awali nilikuwa nienda kushona ngu kwa fundi, asipoisha ambavyo mimi sitaki, basi anachelewa kuikamilisha. Nikasema hapana, ndipo wazo la kuanzisha ofisi hii ya ushonaji na ubunifu wa nguo ili kuondoa usumbufu niliokuwa nikiupata mimi pamoja na watu wengine. Jambo ambalo nimefanikiwa kulitimiza". Anasema Idda Hassan ambae ni Mkurugenzi wa Mikaela Professional Tailors.
Na BMG