Rais Barack Obama amewasihi Wamarekani kuacha kukata tamaa kutokana na wasiwasi wa kibaguzi uliojitokeza.
Akizungumza wakati wa misa ya kumbukumbu ya maafisa polisi watano wa mji wa Dallas waliouawa na mshambuliaji aliyekuwa akilipiza kisasi mauaji ya watu weusi yanayofanywa na polisi, amesisitiza kuwa taifa halijagawanyika kama inavyoonekana.

Rais Obama amekiri kuwa makundi mengi ya watu wachache yamekuwa yakiteseka na ubaguzi.
''.. Marekani, tunajua kwamba upendeleo upo, tunajua hivyo. Aidha uwe Mweusi au mweupe au Mhispania au M'Asia ama mwenye asili ya kuzaliwa America au Mashariki ya kati, tumeiona chuki hiyo katika maisha yetu, tumesikia pia mara kadhaa katika makazi yetu wenyewe...'' alisema Rais Obama.
Lakini hata hivyo amesema Maafisa wengi wa polisi wamekuwa wakifanya kazi ngumu na ya hatari na wanapaswa kuheshimiwa, na sio kukaririwa kwamba wanaupendeleo.
''...Tunajua kwamba maafisa wengi wa polisi wamekuwa wakifanya kazi ngumu na hatari kwa kuzingatia haki na taaluma, wanahitaji kupata heshima yetu na sio kudharauliwa. Na mtu yoyote yule hata kama anania njema, kama atajaribu kuwachafua polisi wote kwamba wanaupendeleo na wabaguzi, kufanya hivyo tutakuwa tunashusha hadhi ya wale maafisa ambao tunawategemea kwa usalama wetu..'' Alisema Rais Obama
Akiwa njiani kuelekea katika mji wa Dallas, Rais Obama aliwapigia simu ndugu za Wamarekani weusi wawili waliouawa katika mashambulio ya hivi karibuni yaliyofanywa na polisi na kusababisha hasira za kufanyika maandamano nchi nzima.