Mwanamuziki kutoka Jamhuri wa Demokrasi ya Congo Koffi Olomide amesafirishwa kwenda mjini kinshasa kutoka Nairobi baada ya kukamatwa Ijumaa usiku.
Olomide alisafirishwa na shirika la ndege la Kenya Airways, kutoka uwanja wa Jomo Kenyatta mwendo wa saa tano unusu asubuhi.

Mwanamuziki huyo alikuwa amekabiliwa na shutuma baada ya kanda ya video kuenea mtandaoni ikionekana kumuonyesha akimshambulia mwanamke uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta Ijumaa asubuhi, muda mfupi baada ya kuwasili.
Mwanamke huyo anadaiwa kuwa mmoja wa wachezaji ngoma wake.
Akiongea katika kituo cha televisheni ya Citizen, muda mfupi kabla ya kukamatwa, Olomide alijitetea na kusema hakukusudia kumshambulia mwanamke huyo.
Alisema alikuwa ameingilia kisa ambacho aliamini ni mtu aliyetaka kumpokonya mmoja wa wachezaji densi wake pochi yake au kulikuwa na vurugu fulani.
Olomide alikamatwa muda mfupi baada ya kumaliza mahojiano katika kituo kimoja cha runinga jijini Nairobi.
Mkuu wa polisi nchini Kenya Joseph Boinnet alikuwa ametoa taarifa na kuwaagiza polisi wachukue hatua.