Kikosi cha Medeama ya Ghana
WAPINZANI wa Yanga katika mchezo ujao wa Kombe la Shirikisho Afrika, Medeama ya Ghana wanatarajiwa kutua nchini kesho tayari kwa mchezo wa Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Yanga katika msimamo wa Kundi A la mashindano hayo, inashika mkia baada ya kutokuwa na pointi, licha ya kucheza mechi mbili wakati Medeama wako katika nafasi ya tatu wakiwa na pointi moja tu.

Mabingwa hao wa Ligi Kuu Tanzania bara walifungwa michezo miwili dhidi ya TP Mazembe (1-0) na dhidi ya MO Bejaia (1-0) wakati Medeama imefungwa mmoja, dhidi ya TP Mazembe (3-1) na kutoka suluhu dhidi ya MO Bejaia.
Kwa mujibu wa tovuti ya michezo ya Ghana, Kocha wa Medeama Prince Ousu leo alitarajiwa kutaja kikosi kitakachokuja nchini kwa ajili ya mchezo huo.
Akihojiwa na mtandao huo, Kocha Ousu alisema ana imani kuwa iwapo ataifunga Yanga katika mchezo huo, kutakuwa na matumaini ya kutinga nusu fainali, kwani tayari wana pointi moja itakayowasogeza mbele zaidi.
Mchezaji anayetakiwa kuangaliwa zaidi katika mchezo huo ni mshambuliaji Malik Akowuah aliyeng’ara katika mchezo wao wa kwanza dhidi ya TP Mazembe, na kumekuwa na taarifa kuwa anatakiwa na timu hiyo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Wakati Medeama ikitarajiwa kuwasili kesho, Yanga inaendelea na maandalizi kuelekea mchezo huo kwenye Uwanja wa Boko Veterani huku wakitamba kuwa wataibuka na ushindi.
Meneja wa timu hiyo, Hafidh Salehe alisema kikosi kinaendelea vizuri na mazoezi na kwamba hali ya mshambuliaji wao Amis Tambwe aliyekuwa amelazwa imeanza kuimarika.
Aidha, tayari vikundi vya ushangiliaji Yanga vimeanza vikao vyao kwa ajili ya kuweka utaratibu wa kuishangilia timu hiyo mwanzo mwisho kwa utaratibu ambao hautaleta vurugu.