Mtuhumiwa wa mauaji, Satoshi Uematsu
Watu 19 wameuawa na wengine 26 kujeruhiwa baada ya kuchomwa kisu katika kituo cha kutunza watu wenye ulemavu Magharibi mwa Mji mkuu wa Japan, Tokyo.
Tukio hilo linaelezwa kuwa moja ya mauaji ya idadi kubwa ya watu nchini Japan tangu Vita ya Pili ya Dunia.

Wanaume tisa na wanawake kumi wenye umri kati ya miaka 18 na 70 wameuawa katika shambulio hilo.
Ofisa wa Kikosi cha Zimamoto, Satomi Kurihara amethibitisha kutokea mauaji hayo katika kituo cha Tsukui Yamayurien katika mji wa Sagamihara kilichopo karibu Kilometa 40 kutoka Tokyo.
Maafisa wa Jimbo la Kanagawa wasema katika mkutano na waaandishi wa habari kuwa kijana mwenye umri wa miaka 26 Satoshi Uematsu ambaye alikuwa mfanyakazi wa kituo hicho hadi Februari mwaka huu aliingia kituoni baada ya kuvunja dirisha mapema leo.
Ripoti za polisi zimesema Uemattsu alijipeleka mwenyewe kituo cha polisi Sagamihara akiwa na kisu na nguo zenye damu na kukiri kutekeleza mauaji.
Polisi wamesema muuaji huyo alipeleka barua kwa wanasiasa Februari mwaka huu akitishia kuua mamia ya watu wenye ulemavu.
"Lengo langu ni kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapotea duniani ambako ni vigumu kwao kuishi nyumbani na kushiriki masuala ya jamii bila wasaidizi", ilisema sehemu ya barua hiyo.
Waziri wa Nchi anayeshughulikia Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri la Japan, Yoshihide Suga amesema: "Ni tukio linaloshtua moyo lililopoteza maisha ya watu wengi wasio na hatia." Alihifadhiwa hospitali kwa karibu wiki mbili kabla ya kuruhusiwa.