KIONGOZI wa Jumuiya ya Mabohora Duniani, Dk Syedna Mufaddal Saifuddin amesema wataendelea kuisaidia Tanzania kutokana na kuridhishwa na utendaji kazi wa serikali ya Awamu ya Tano inayoendelea kuhakikisha nchi inakuwa na amani.
Pia alitangaza mkutano mkuu wa dunia wa jumuiya hiyo utafanyika Dar es Salaam, Oktoba mwaka huu.

Alisema hayo jana mjini hapa alipowasili Uwanja wa Ndege wa Dodoma kwa ziara ya siku 14 nchini ambako alipokewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Augustine Mahiga, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbanana viongozi mbalimbali wa Jumuiya ya Waislamu Tanzania (BAKWATA) wakiongozwa na Mufti wa Tanzania, Shehe Mkuu Abubakar bin Zubeiry.Alisema Tanzania ni moja ya nchi za kujivunia kutokana na amani iliyopo na kama jumuiya wataendelea kusaidia nchi katika nyanja mbalimbali ikiwemo elimu.
“Nitaendelea kuhimiza jumuiya yetu iendelee kutoa misaada kwa ajili ya kuboresha elimu nchini,” alisema.
Pia aliahidi kutoa Dola za Marekani 53,000 (Sh milioni 111) kwa serikali na dola 21,000 (Sh milioni 44) kwa Bakwata, fedha ambazo zitatumika kwa shughuli mbalimbali za maendeleo.
Naye Balozi Mahiga, akizungumza kwa niaba ya Rais John Magufuli alisema wamekuwa wakiridhishwa na jinsi jumuiya hiyo inavyoendelea kutunza amani, umoja na masikilizano huku akitolea mfano jinsi walivyojitolea madawati kwa shule za Dar es Salaam.
Alisema wataendelea kushirikiana na jumuiya hiyo kutokana na wao kuwa wafanyabiashara na Serikali ya Tanzania kipaumbele chake ni kuwa nchi ya viwanda.
Alisema katika msingi wa lengo la uchumi wa viwanda, Jumuiya ya mabohora imejikita katika viwanda mbalimbali kama Dar es Salaam, Mwanza na maeneo mengine.
Mwenyekiti Msaidizi wa Jumuiya ya Mabohora Mkoa wa Dar es Salaam, Zainuddin Adamjee alisema wamepata faraja kubwa kuona baada ya miaka 43, Rais Magufuli anatamka serikali kuhamia Dodoma katika kutimiza azma ya Rais wa Kwanza, Julius Nyerere aliyetangaza serikali kuhamia Dodoma mwaka 1973. Alisema sasa Dodoma mpya inakwenda kujengwa.