Serikali ya Marekani imeahidi kuipatia Tanzania dola milioni 407 fedha za msaada miezi kadhaa baada kukatiza ufadhili kama huo kufuatia uchaguzi inaodai ulikiuka demokrasia.
Shirika la Marekani Millenium Challenge Corporation MCC lilifutilia mbali msaada huo wa kitita cha dola milioni 473 mnamo mwezi Machi baada ya uchaguzi katika kisiwa cha Zanzibar kudaiwa kutozingatia maadili ya uhuru na uwazi.

Marekani ilisema wakati huo kwamba misaada mingine hatahivyo haitaathiriwa.
Haji Ssemboja profesa wa maswala ya kiuchumi alikiambia chombo cha habari cha Reuters kwamba usaidizi huo mpya unamaanisha kwamba Marekani inafurahishwa na mabadiliko yanayofanyika serikalini.
''Ijapokuwa mpango wa MCC na ufadhili huu ni mipango miwili tofauti ,msaada huu ni ishara kwamba Tanzania inaelekea katika njia nzuri'',alisema.
Ubalozi wa Marekani umesema kuwa fedha hizo zitatolewa mwaka huu ili kusaidia afya,kilimo,mali asili,usimamizi,elimu,kawi na uongozi wa kidemokrasia.