Wanajeshi 17 wa Muungano wa Afrika wanaohudumu nchini Somalia chini ya mwavuli wa AMISOM wamefikishwa mahakamani mjini Mogadishu kujibu mashtaka ya wizi.
Wanajeshi hao kutoka Uganda walikamatwa kwa tuhuma za wizi wa bidhaa za kijeshi ikiwemo mavazi silaha na mafuta.
Mahakama ya kijeshi ya Uganda iliandaa kikao hicho maalum mjini Mogadishu kufuatia shinikizo kutoka kwa serikali ya Somalia iliyowakamata.
Kikao hicho ni cha kwanza kabisa kuwahi kuandaliwa nje ya Uganda.
Wanajeshi wa Uganda waliingia Somalia yapata miaka 9 iliyopita.
Kesi yao inasikizwa na maafisa 7 katika kipindi cha siku tatu kuanzia leo.

Image captionKikao hicho ni cha kwanza kabisa kuwahi kuandaliwa nje ya Uganda.

Mwanajeshi mmoja tayari amehukumiwa kifungo cha mwaka mmoja gerezani baada ya kukiri makosa yake.
Atatumikia kifungo chake nchini Somalia.
Uganda ndio taifa lililochangia idadi kubwa zaidi ya wanajeshi nchini Somalia chini ya mwavuli wa AMISOM