Takriban watu 17 wamefariki nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kufuatia maandamano yanayomtaka rais Joseph Kabila kujiuzulu.
Watatu kati yao walikuwa maafisa wa polisi ambao mmoja wao alichomwa akiwa hai kulingana na waziri wa maswala ya ndani Evariste Boshab.

Waandamanaji waliweka vizuizi na kuchoma magari katika mojawapo ya barabara kuu mjini Kinshasa.
Maafisa wa polisi walirusha vitoa machozi kuwatawanya waandamanaji .
Mmoja ya mashahidi amesema kuwa maafisa wa polisi waliwafyatulia risasi waandamanaji.
Miili ya watu waliofariki ilionekana ikiwa imetapakaa katika barabara baada ya maandamano kuisha.
Tume ya uchaguzi nchini humo ilitarajiwa kutangaza siku ya uchaguzi unaotarajiwa mwezi Novemba siku ya Jumatatu,lakini amsema kuwa haiwezekana kufanyika wakati huo.
Upinzani unasema kuwa bwana Kabila anajaribu kuchelewesha uchaguzi ili kusalia madarakani kupita kipindi cha muhula wake wa pili unaokamilika mwezi Disemba.