Ripoti mpya iliyotolewa na shirika moja lisilo la kiserikali lenye makao yake makuu nchini Uswizi liitwalo Public Eye, limezishutumu kampuni za utengenezaji bidhaa kwa kuhusika kwao katika biashara ya mafuta na mataifa ya Afrika, ambayo ina kiwango cha juu cha sumu ambayo ni kinyume na sheria kutumika barani Ulaya.

Ripoti hiyo iliyopewa jina Dirty Diesel, inasema kwamba wauzaji wa mafuta aina ya dizeli wanatumia kanuni dhaifu ili kupata faida kwa kuuza mafuta "machafu" kwa watumiaji barani Afrika.
Ripoti hiyo inadai kuwa baadhi ya sampuli za dizeli zilizokusanywa kutoka kwa mataifa manane ya Afrika zina kiasi fulani ya chembechembe ya madini aina ya sulphur ambayo ni mara 300 zaidi ya kiwango kinachokubalika barani Ulaya.
Hata ingawa hii ipo ndani ya mipaka ya kisheria iliyobuniwa na mataifa mbalimbali, moshi kutoka kwa dizeli ya aina hiyo unaweza kuongeza maradhi ya kupumua kama vile pumu na ugonjwa wa mapafu, yanayowasumbua watu katika mataifa mengi.

Chembe chembe za Sulphur katika moshi wa mafuta ya dizeli zimehusishwa na matatizo mengi ya kiafya kwa binadamuImage copyrightAFP
Image captionChembe chembe za Sulphur katika moshi wa mafuta ya dizeli zimehusishwa na matatizo mengi ya kiafya kwa binadamu

Ripoti hiyo inasema kwamba kampuni nne za uuzaji bidhaa nchini Uswizi, Vitol, Oryx na Lynx Energy, Trafigura pamoja na Addax, zimefaidi pakubwa katika biashara hiyo kama wanahisa katika makampuni ya usambazaji.
Lakini makampuni mawili, Trafigura na Vitol, yanasema kuwa ripoti hiyo ni potofu na kwamba yanaendesha biashara yao inavyostahili na moja kwa moja kutoka kwa wauzaji wanaofanya kazi chini ya mipaka mikali ya kisheria katika nchi hizo.
Kati ya makampuni ya usambazaji yaliyotajwa, matatu yamejibu taarifa hiyo, huku yakisema kwamba yanakidhi mahitaji ya udhibiti wa soko na hayana nia ya kuongeza kiwango cha madini ya sulphur kwenye bidhaa zao.