Serikali nchini Gabon imewakamata zaidi ya watu elfu moja katika siku ya pili ya ghasia zilizozushwa na wapinzani waliokuwa wakipinga matokeo ya uchaguzi wa Rais uliofanyika nchini humo Jumamosi iliyopita.
Ripoti kutoka katika mji mkuu wa Gabon Libreville, zinasema kuwa watu watatu wameuawa katika ghasia hizo.

Rais Ali Bongo ambaye ndiye aliyetangazwa mshindi katika uchaguzi huo amewalalamikia wafuasi wa upinzani ambao walimiminika mitaani siku ya Jumatano na kuchoma moto bunge la nchi hiyo.
Amesema demokrasia haiwezi kupatikana kwa njia kama hizo.
Akizungumza na vyombo vya habari, Rais Bongo amesema ghasia zilizotokea baada ya uchaguzi sio za kidemokrasia.
Amesisitiza kuwa uchaguzi umeisha, hivyo yawapasa kuungana pamoja na kuachana na shutuma zote za wakati wa kampeni, ili kuweza kupata maridhiano.
Mpinzani wa Rais Bongo katika uchaguzi huo, kiongozi wa Upinzani Jean Ping ameiambia BBC kwamba Jumatano usiku helikopta za serikali zilivamia makao makuu yake na watu wawili kuuawa, huku yeye na familia yake wakijificha.
Wafuasi wa upinzani wameilalamikia serikali kwamba imefanya hila katika uchaguzi huo na kumtaka Rais Bongo kujiuzulu.
Katika hatua Umoja wa Mataifa, Marekani na Ufaransa wametoa wito kwa watu kujizuia na kuwepo kwa uwazi kuhusiana na matokeo