Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako
WIZARA ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi imezifuta shule za awali, msingi na sekondari nchini ambazo hazijasajiliwa zaidi ya 40 kuanzia Julai mwaka jana.
Awali kuanzia Julai hadi Desemba mwaka jana, waligundua kuwepo kwa shule 35 zisizosajiliwa na kuzifuta, jambo lililofanya kutangaza shule zote ambazo hazijasajiliwa kujisalimisha ili kusajiliwa.

Kaimu Mkurugenzi wa Usajili wa Shule katika wizara hiyo, Khadija Mcheka alisema Mei mwaka huu baada kuzipa miezi miwili shule ambazo hazijasajiliwa kufanya hivyo, walizifungia shule nyingine 12.
Mcheka alisema shule zinaweza kufutwa kwa sababu mbili zikiwamo zilizosajiliwa, lakini zikakiuka vigezo ambazo zikitimiza vigezo zinaweza kuomba upya usajili na kupewa.
“Lakini aina ya pili ni zile ambazo hazijasajiliwa na zinaendeshwa kinyume cha sheria ambazo nazo zikifuata taratibu zikatimiza vigezo zinaweza kupewa usajili,” alifafanua Kaimu Mkurugenzi wa Usajili wa Shule.
Alisema katika kipindi hicho mpaka Agosti mwaka huu baada ya tangazo la kuwataka kusajiliwa shule za awali nne, zile za awali na msingi 105 na sekondari 19, walifika wizarani kwa ajili ya kupata taratibu za usajili ambapo zipo zilizosajiliwa na nyingine kupewa vibali.
Alisema katika usajili, kuna wapo waliokidhi viwango na wengine waliopatiwa maelekezo na kupatiwa vibali vya kutumia majengo yaliyopo huku wengine wakipewa vibali vya kujenga majengo ya shule kabla ya kupata usajili.
Alisema kwa shule walizozifungia, waliwaandikia barua za kuwafungia na kuwataka kuhakikisha wanawatawanya wanafunzi katika shule zilizosajiliwa kwa gharama zao bila kuwaathiri wanafunzi.
Alitaja shule zilizofungiwa kwa kuendesha shughuli zake bila usajili kuwa ni shule za awali na msingi za Must Lead ya mkoa wa Pwani, na za mkoa wa Dar es Salaam ni Brainstorm, Pax, Lassana, Grace, Rose Land, Julius Raymod, St Thomas, Mary Mother of Mercy, Noble Sinkonde, Immaculate Heart of Mary, St Columba, Corner stone, Dancraig, Mwalimu Edward Kalunga, Edson Mwidunda, Gisela, Kingstar, St Columba awali, Bilal Muslim, Thado, Hocet , Elishadai, Lawrance Citizen, Comrade, Dar Elite Preparatory na Golden Hill Academy na Hekima.
Nyingine ni Pwani Islamic, St Kizito na Rwazi Encysloped za Kagera, Dancraig na Qunu za Pwani, Hellen’s ya Njombe, Joseph ya Arusha, Samandito na Maguzu za Geita. Alizitaja shule za Sekondari zilizofungiwa kwa sababu hiyo kuwa ni Hananasif, Elu, Hocet, Safina za Dar es Salaam na Namnyaki ya Iringa.
Aidha, Shule ya Fountain Gate ya jijini Dar es Salaam imefungiwa kwa kuendesha bweni bila kibali.
“Baada ya kutoa tangazo kutokana na kubaini kuwapo shule nyingi zisizosajiliwa, wapo waliojitokeza na nyingine tumezifungia kutokana na kutokidhi viwango vya usajili lakini pia tunaamini wapo waliojificha wakiendelea kutoa huduma,” alisema Mcheka na kuwaagiza wakaguzi katika kanda na wilaya, kufanya ukaguzi na kutoa taarifa kwa zile ambazo hazijafungiwa na ikithibitika hazijasajiliwa, kuzifungia mara moja.
Alisema utaratibu uliopo kwa kuhakikisha shule zote zinasajiliwa kulingana na viwango stahili kwa lengo la kutoa elimu bora ni wakaguzi wa kanda, mikoa na wilaya kwa kushauriana na waratibu wa elimu katika kata, kuhakikisha shule yoyote inayochomoza, wanaifuatilia na kuwapa ushauri wa kufuata taratibu za usajili kwa kukidhi viwango stahili.
Alisema wamekuwa wakigundua kuwapo kwa shule, ambazo hazijasajiliwa kutokana na wakati wa mitihani idadi ya wanafunzi inazidi tofauti na walivyosajiliwa na kubainika kuwa wapo waliokuwa wakisoma katika shule, ambazo hazijasajiliwa wanawapeleka katika shule zilizosajiliwa.
“Kuna wenye shule ambazo hazijasajiliwa wakati wa mitihani wanakuja kuomba wanafunzi kufanya mitihani hivyo kuleta usumbufu wa kuwatawanya kwenye shule zilizosajiliwa na kwenda kuwakagua ili kuweza kusajiliwa,” alifafanua.
Msajili huyo alisema madhara yanayotokana na mwanafunzi kusoma shule ambazo hazijasajiliwa ni pamoja na haitajulikana mtoto anachosoma kwani haitajulikana mitaala wanayotumia kutokana na kukosa usajili, hivyo kushindwa kufanya mitihani. Pia mazingira ya shule na mpangilio wake, haitaendana na matakwa ya serikali ya kutoa elimu bora kwani mmiliki atafanya kile anachotaka.
Mei mwaka huu, wizara hiyo ilizipa miezi miwili hadi Julai 30, mwaka huu kuhakikisha shule zote ambazo hazijasajiliwa zinajisajili kabla ya serikali kuzifunga.
Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Dk Leonard Akwilapo alisema ifikapo Julai 30, mwaka huu, mmiliki wa shule itakayobainika kutosajiliwa ikiwemo zitakazokosa vigezo vya kusajiliwa, atapaswa kuhamisha wanafunzi waliopo kwa gharama zake.
Alipoulizwa ni shule ngapi ambazo zinajiendesha bila kusajiliwa, Kaimu Mkurugenzi Mcheka alisema tatizo kubwa lipo kwa shule za awali na msingi.