BARAZA la Taifa la Uwezeshaji limesema fedha Sh milioni 50 za kila kijiji zilizoahidiwa na Rais John Magufuli, utaratibu wa utoaji wake unaandaliwa na mapema mwanzoni mwa mwaka ujao zitakuwa zimetoka.
Mkurugenzi wa Mifuko ya Uwezeshaji katika Baraza hilo, Edwin Chrisant ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam katika juma la benki za maendeleo vijijini (Vicoba) na kuongeza kuwa fedha hizo zitakwenda kwa wananchi walioko katika vikundi peke yake.

Maadhimisho hayo ya Vicoba yameandaliwa na Asasi iliyo ya kiserikali ya kijamii ya Maendeleo na Uchumi inayojishughulisha kutoa elimu na mafunzo kwa wanachama wa vyama hivyo (SEDIT).
Kuhusu fedha hizo za ahadi za Rais Magufuli, mkurugenzi huyo alisema serikali itakamilisha mpango wa fedha hizo kwa kila kijiji na zitakwenda kwa wale walioelimishwa namna nzuri na utaratibu wa fedha ili zifanye kazi iliyokusudiwa.
Alisema utoaji wa fedha hizo kwa kipindi hicho utakuwa wa aina tofauti na zitahakikishwa zinawafikia wananchi wa kipato cha chini kwa masharti yaliyo rahisi, ikiwa ni pamoja na kuwatambua zaidi walioko katika vikundi.
Alisema Watanzania wenye dira ya shughuli za kiuchumi suluhu ya kufikia malengo yao ni kupata mtaji, jambo ambalo Baraza la Uwezeshaji linashughulika nalo ili kupanua wigo wa maendeleo nchini.
Mkurugenzi wa SEDIT, George Sweveta alisema taasisi zinazotoa elimu kwa Vicoba zimepata sera mpya ambapo muda wowote wanaweza kupata sheria ambayo inaweza kuwalinda na kuwawezesha kukaa meza moja na serikali kwa ajili ya maendeleo ya vyama hivyo.