Tume ya haki za binadamu nchini zimbabwe imesema kuwa watu wanaounga mkono upinzani, walio kwenye maeneo yenye ukame wamenyimwa misaada ya chakula na chama tawala cha ZANU-PF.

Mwenyekiti wa bodi maalum Elasto Mugwadi, amesema kuwa kwa sasa uchunguzi umebainisha kuwa watu wanaounga mkono upande wa upinzani wanaambiwa waziwazi kuwa hawatopewa msaada wowote wa chakula na inaarifiwa kuwa watu wengi wameathirika kutokana na hali hiyo.Taarifa ya serikali inaonyesha kuwa nusu ya wakazi wa vijijini wamekumbwa na njaa, jambo linalochochea kupingwa kwa utawala wa rais Mugabe.
Wakati huo huo mahakama kuu nchini humo imebatilisha marufuku ya maandamano yaliyokatazwa na polisi kwenye mji mkuu wa Harare. Ambapo marufuku hiyo ilidumu kwa muda wa wiki mbili.
Wanaharakati wanne wanaopinga utawala wa rais Mugabe ndiyo waliwashilisha pingamizi mahakamani kupinga uamuzi wa polisi kupiga marufuku maandamano kwenye mji mkuu wa Harare.
Hakimu wa mahakama kuu ya nchini humo amesema kuwa marufuku hiyo ya polisi ilikuwa batili. Siku za hivi karibuni kumekuewa na ongezeko la wimbi la maandamano nchini Zimbabwe, wakiandamana kuhusu mdororo wa uchumi nchini humo.
Maandamano makubwa yanaratibiwa na wanaharakati kupitia mitandao ya kijamii.