WATUMISHI 34 wa mahakama wakiwemo mahakimu 11, wamefukuzwa kazi kutokana na makosa mbalimbali ya kinidhamu.
Aidha, Tume ya Utumishi wa Mahakama inaendelea kujadili hatma ya mahakimu 30, waliokuwa wanatuhumiwa kuhusika na rushwa na kushinda zao mahakamani ili kuangalia kama walifanya makosa ya kinidhamu.

Jaji Mkuu, Mohammed Chande Othman alisema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kupokea taarifa za ukaguzi wa mahakama pamoja na uendeshwaji wa mashauri.
Othman alisema watumishi hao, wamefukuzwa kutokana na uamuzi wa kikao cha Tume ya Mahakama, kilichofanyika Agosti 18, mwaka huu baada ya kushughulikia masuala mbalimbali ya kinidhamu.
“Tumewafukuza mahakimu wakazi wafawidhi, mahakimu wa mahakama za Mwanzo za Rombo, Temeke, Bahi na Chamwino na watumishi wengine 23. Hii ni idadi ndogo ambayo ni sawa na asilimia 0.005 ya wafanyakazi wote lakini kwa mahakama ni doa kubwa,” alisema Jaji Mkuu.
Alisema mahakimu hao wamefukuzwa kwa makosa mbalimbali ya kinidhamu, ikiwemo kutumia muhuri wa mahakama kinyume cha taratibu, kuathiri utendaji wa haki kwa kumsaidia mtu kufungua kesi moja katika mahakama mbili pamoja na kufungua kesi ya mirathi bila kuwa na hati ya kifo.
Aliongeza kuwa kuna makosa ya kisheria ambayo jaji au hakimu akikosea kutumia kifungu cha sheria hawajibishwi, lakini kuna makosa ya kinidhamu ambayo yanaondoa sifa ya kuwa hakimu au jaji.
Kuhusu mahakimu walioshinda kesi za rushwa mahakamani, Jaji Chande alisema mahakama inaweza isiwakute na hatia, lakini Tume itaangalia kama walifanya vitendo vya ukosefu wa nidhamu na kuwawajibisha.
Aidha, alisema mahakimu wengine 32 waliokuwa wanakabiliwa na kesi za jinai na kushinda kesi mahakamani, wanafunguliwa mashitaka ya kinidhamu katika Kamati ya Maadili ya Maofisa wa Mahakama kwa sababu inawezekana hawajapatikana na hatia ya kosa la jinai, lakini kama kuna vitendo vya ukosefu wa maadili watawawajibisha kimaadili.
Mahakama Maalumu ya Ufisadi na Uhujumu Katika hatua nyingine, Mahakama Maalumu ya Ufisadi na Uhujumu Uchumi imeanza rasmi na wiki ijayo Kanuni za Uendeshaji wa mahakama hiyo, zinatarajiwa kuchapishwa. Jaji Mkuu Othman alisema mahakama hiyo, imeanza rasmi Julai 18 mwaka huu baada ya Rais John Magufuli kusaini sheria ya uanzishwaji wa mahakama hiyo.
“Wiki ijayo tutachapisha kanuni mbalimbali za uendeshwaji wa mahakama hiyo, ikiwemo jinsi ya kulinda mashahidi pamoja na taratibu za ufunguaji wa kesi,” alisema Othman.
Alisema mahakama hiyo itakuwa na majaji wa kutosha ili kufanya kazi kwa uadilifu na kumaliza kesi kwa wakati, pia haitakuwa ikiahirisha kesi mara kwa mara.
Kuhusu utendaji kazi wa mahakama, Jaji Mkuu alisema mahakama haiwezi kutoa haki kama itakuwa inajificha au kuendeshwa kwa siri, ndiyo maana kwenye maboresho ya mahakama, wameamua kuwapa fursa wananchi kutoa mapendekezo au kero zao kupitia namba za simu pamoja na barua pepe.
Kesi za uchaguzi Awali akiwasilisha taarifa za utendaji wa Mahakama Kuu, Mahakama za Hakimu Mkazi, Wilaya na za Mwanzo, Msajili wa Mahakama Kuu, Ilvin Mugeta alisema baada ya uchaguzi, walipokea kesi 247 za uchaguzi, 53 za kupinga matokeo ya ubunge na 194 za udiwani.
Mugeta alisema tayari wameshamaliza kesi 234, zimebaki 13, lakini hadi kufikia Desemba mwaka huu kesi zote zitakuwa zimemalizika.
Aidha, alisema tathmini waliyoifanya inaonesha kesi zilizopo zinawiana na mahakimu, na kama watawezeshwa kwa vifaa vya kutendea kazi hadi Desemba mwaka huu watamaliza kesi zote zilizofunguliwa mwaka huu.
Mahakama ya Rufaa Kwa upande wake, Msajili wa Mahakama ya Rufaa, John Kahyoza alisema kiwango cha kumaliza mashauri katika Mahakama ya Rufaa kimeongezeka, pia wana lengo la kuhakikisha nakala za hukumu zinapatikana siku hukumu na ndani ya siku tatu zitapatikana kwenye tovuti ya Mahakama ya Tanzania.
Aidha, aliwaomba wananchi watoe ushirikiano ili rufaa zisikilizwe na kuisha mapema, kwa sababu kuna watu wanashindwa kufika mahakamani bila sababu za msingi au kutoa visingizio jambo linalosababisha rufaa zao kuchelewa.
Umuhimu wa mahakama Katika hotuba yake kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria Februari 4, mwaka huu, Rais Magufuli alisema anaitegemea sana Mahakama na aliwaambia majaji na mahakimu nchini kuwa:
“Nawaomba waheshimiwa majaji na waheshimiwa mahakimu, muitangulize Tanzania kwanza. Mkiitanguliza Tanzania kwanza tutaweza kufika mbali na tutaweza kuwasaidia watanzania wengi. Nimeamua nchi iende, na itaenda. Anayefikiri ataikwamisha, atakwama yeye kwa sababu Mungu yuko pamoja na mimi. Na watu ninaowategemea sana ni Mahakama. Mahakama unafunga kila mmoja. Hata Rais nikitaka kufungwa na Mahakama, nafungwa. Mbunge anafungwa, nani anafungwa, nyinyi ndio wenyewe”.