Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Ummy Mwalimu (kushoto) akiongoza na mwenyeji wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida mara baada ya kuwasili kwenye ofisi za ESRF kufungua warsha ya nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs)  iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International.
  Mkurugenzi Mkazi Shirika la kimataifa la kusaidia wazee (Help Age International), Amleset Tewodros (wa kwanza kushoto) akifafanua jambo kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Ummy Mwalimu (wa pili kulia) ofisini kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida (katikati). Wengine kushoto ni Mkurugenzi wa Kupunguza Umaskini na Kuinua Uchumi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Anna Mwasha na Mkurugenzi Mkazi Msaidizi wa Shirika la kimataifa la kusaidia wazee (Help Age International), Smart Daniel (wa pili kushoto).
 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida akitoa neno la ukaribisho kwa mgeni rasmi na washiriki wa warsha ya nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs)  iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.
 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akifungua warsha kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International na kufanyika katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.
 Mwakilishi wa Jukwaa la Wazee Tanzania, Samson Msemembo (85) akizungumzia changamoto wanazokutana nazo wazee katika vituo vya huduma za afya kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu (katikati), Kaimu Kamishna Ustawi wa Jamii Bw.Rabikira Mushi kutoka Wizara ya Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (kushoto) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida waliopo meza kuu.
 Mtafiti Mkuu Mshiriki kutoka Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF) na Mhadhiri Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Oswald Mashindano akizungumzia nafasi ya wazee katika sera ya kitaifa kwenye warsha kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.
 Mkurugenzi Mkazi Shirika la kimataifa la kusaidia wazee (Help Age International), Amleset Tewodros akishiriki kutoa maoni kwenye warsha kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International na kufanyika katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida akifafanua jambo kwenye warsha ya nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs)  iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International. Kushoto ni Mkurugenzi Mkazi Shirika la kimataifa la kusaidia wazee (Help Age International), Amleset Tewodros.
  Mshauri wa Masuala ya Ushirikiano wa Kanda ya Afrika Mashariki, Kati na Magharibi wa Shirika la Help Age International, Roseline Kihumba akizungumzia hali ya uzee na wazee duniani na ushirikishwaji wa wazee katika maendeleo endelevu kwenye warsha ya nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs)  iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International.

Mkurugenzi wa Kupunguza Umaskini na Kuinua Uchumi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Anna Mwasha akichangia mada kwenye warsha ya nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International.
  Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Uchambuzi wa Sera na Utafiti wa Wizara ya Fedha na Mipango, Mudith Cheyo akifafanua jambo kwa washiriki wa warsha kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs)  iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International.
 Mkurugenzi wa Mtandao wa Watu Waishio na Virusi vya Ukimwi Tanzania (SHDEPHA), Joseph Katto akizungumzia changamoto zinazowakabili wazee wanaoishi na VVU katika kupata huduma mbalimbali nchini kwenye warsha kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International na kufanyika katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya washiriki waliohudhuria warsha kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International na kufanyika katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam
  Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Ummy Mwalimu akizungumza na waandishi wa habari nje ya ukumbi wa mikutano wa ESRF wakati wa warsha kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) iliyoandaliwa na ESRF kwa kushirikiana na Shirika la Help Age International
 Picha ya pamoja

Na Mwandishi wetu
SERIKALI ya Tanzania imeshauriwa kuhakikisha kwamba kunakuwapo na ushirikishaji wa wazi wa wazee katika sera na mipango ya maendeleo.
Aidha imetakiwa kutoa nafasi kwa wazee katika utekelezaji wa miradi yake ya maendeleo, jamii na mazingira.
Kauli hizo zimetolewa na washiriki  wa warsha ya nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu ,SDGs ambayo imeingizwa katika mipango ya maendeleo ya taifa.
Wakiongozwa na mada mbalimbali zilizotolewa na wataalamu mbalimbali kama Dk Oswald Mashindano, Danford Sango,  Ahmed Makbel, Dk. Ntuli Kapologwe washiriki walisema kwamba ingawa Tanzania ina sera nzuri kuhusu wazee utekelezaji wake umekuwa wa kusuasua kutokana na kukosekana kwa utashi.
Aidha walisema kwamba kukosekana kwa sheria ya wazee kunawafanya wazee hao kunyanyasika hasa katika masulaa ya kiuchumi na kiafya.
Joseph Kato (62) ambaye alisema kwamba amekuwa akiishi na UKIMWI tangu ujana wake hadi sasa ameingia rasmi katika rika la wazee, anasema kwamba sera za nchi hasa za afya haiztoa umuhimu kwa magonjwa kama Ukimwi.
Aidha alisema kwamba wazee wakiwa na afya zao wamekuwa wakipuuzwa katika suala la uchumi kwani ukiwa unaishi na Virusi vya Ukimwi ukienda benki hupewi mikopo na pia ukiwa mzee hupewi mikopo.
Alisema kama sera ni kuhakikisha hakuna anayeachwa katika safari za utekelezaji wa maendeleo endelevu ipo haja kwa serikali kuhakikisha kwamba wazee hawanyanyaswi na wanasaidiwa kuwezeshwa kiuchumi.
Mshiriki mwingine aliyejitambulisha kama Mama Koku alisema kwamba ngazi za chini za utekelezaji zimekuwa hazitoi kipaumbele kwa wazee japo serikali kuu katika mipango yake imeonesha nini kinachotakiwa kufanywa na kila mmoja katika nafasi ya kuhudumia wazee.
Alisema upo mkakati wa mwaka 2007 hadi 2025 ambao umeonesha utekelezaji wa huduma kwa makundi tete lakini wakurugenzi wa halmashauri hawaweki wazee kama kipaumbele chao wakisingizia serikali kuu.
Hata hivyo amesema wakati umefika kwa serikali kufuatilia mkakati huo kwa lengo la kuwabana wahusika ili kipaumbele kwa wazee kiwepo.
Amesema maofisa mipango wengi wanakwepa kuweka kipaumbele kwa dai kuwa fedha wanazoletewa ukomo wake hauruhusu kuwaingiza wazee huku wengine wakidanganya kwamba serikali kuu ndio imeondoa msaada kwa wazee.
Naye Ishaka Msigwa kutoka Ruvuma alisema kwamba tatizo kubwa la kuhudumia wazee sio sera kwani ipo ila dhamira ndio haipo. Alisema wazee wanataabika sana katika suala la uchumi na kwamba ipo haja sheria ya wazee ikatungwa ili kuwasaidia kuondokana na adha ya kukataliwa wakati wa kutafuta mikopo ya kuwainua kiuchumi.
Alisema asilimia 50 ya mayatima wanakaa na wazee vijijini na kitendo cha kuwanyima ushiriki wa uwezeshaji unawatesa.
Pamoja na malalamiko hayo ya wazee  ambayo yalijikita katika kuwa na kipato cha uhakika na suala la upatikanaji wa matibabu, serikali ilisema imekamilisha utaratibu wa utoaji wa pensheni kwa wazee Tanzania bara na kinachosubiriwa kwa sasa ni utekelezaji wake.
Waziri wa Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu  akifungua warsha hiyo kuhusu nafasi ya wazee katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) alisema hata hivyo serikali itaanza kutoa posho hizo kwa wazee wa miaka 70  kwenda juu na badae watashuka hadi katika umri unaokubalika.
Alisema wamejifunza kutoka Zanzibar na wanaona hapo ni eneo jema la kuanzia.
Aidha alisema kwamba bado anaendelea na juhudi zake za kutaka sheria ya wazee itungwe kwa kuwa ipo sera inayohusu wazee.
Kwa hesabu za karibuni Tanzania inawezee zaidi ya milioni 2.
Pamoja na kuzungumzia suala la malipo ya pensheni ambapo alisema suala hilo kwa sasa lipo Hazina, waziri huyo alirejea msisitizo wake wa kutaka wazee watibiwe bila malipo.
Alisema serikali ya awamu ya tano ni serikali ya utekelezaji na kwamba suala la tiba bure kwa wazee ni suala la sera na wala si utashi.
Akizungumza kwa kina masuala yanayogusa wazee kama yalivyotolewa kwa sauti na mzee Samson Msemembo (85), Waziri Ummy alisema kwamba serikali inatambua changamoto zinazowakumba wazee na itazifanyia kazi kuhakikisha kwamba zinapatiwa majibu.
Mzee Msemembo kutoka Jukwaa la wazee Tanzania, alisema kwamba wazee wamekuwa wakinyanyasika katika sekta ya afya na uchumi wakibaguliwa na kunyimwa fursa za kuishi kwa furaha.
Akizungumza kuhusu kero zilizoelezwa katika warsha hiyo iliyoendeshwa kwa pamoja katika Taasisi za Tafiti za Kiuchumi na Kijamii nchini (ESRF) na taasisi ya kimataifa ya kusaidia wazee Help Age, Waziri Ummy alisema serikali inataka wazee wawe na  kipato cha uhakika na kupewa matibabu.
Amesema hakubaliani na suala la wazee kukosa matibabu na kutaka wakurugenzi wote wa halmashauri kuhakikisha kwamba wazee wanaingizwa katika mfumo wa matibabu wa CHF au wanapewa kadi maalumu ya matibabu bure.
Alisema kwamba haingii akilini kuona kwamba wazee sita katika watu 100 wanakosa kutibiwa kwa dai la kukosekana kwa fedha wakati sera zipo zinazotaka watibiwe bure.
Akizungumzia tatizo  la Hospitali ya Taifa Muhimbili kutotibia wazee alisema kwamba atalishughulikia tatizo hilo kwani haliingii akilini mwake:“Watumishi, vifaa, kila kitu ni cha serikali inakuaje wazee wasitibiwe” alihoji Waziri Ummy .
Akizungumzia suala la kukuza uchumi wa wazee alisema kwamba atamwandikia barua Rais Magufuli ili aweze kutoa agizo la asilimia 2 katika mapato ya ndani ya halmashauri kuchochea uchumi kwa wazee.
Alisema kuna asilimia 5  zimetengwa kwa vijana na wanawake pia 5 na haoni sababu zisitengwe asilimia 2 kwa ajili ya wazee.
Katika warsha hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa ESRF Dk Tausi Kida alisema kwamba warsha hiyo imelenga kusaidia wadau mbalimbali kutambua masuala ya wazee katika mipango ya maendeleo kuanzia ngazi za chini ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu ya dunia.