Taifa la Tanzania limefutilia mbali usajili wa meli kadhaa za Korea Kaskazini kwa kupeperusha bendera za taifa hilo kinyume na sheria.
Waziri wa maswala ya kigeni wa Tanzania Augustine Mahiga aliambia BBC kwamba meli hizo zilionekana hivi karibuni katika bahari hindi eneo ambalo halipo mbali na Tanzania.

Hatahivyo hakutoa idadi kamili ya meli hizo.
''Meli za Korea Kaskazini zilipigwa marufuku na Umoja wa Mataifa na hazikuruhusiwa kusafiri ama hata kutia nanga'',alisema Mahiga.
''Kwa hivyo meli hizi zimekuwa zikijaribu kutafuta njia kukiuka vikwazo hivyo ili kuweza kuendelea na biashara zao,na mbinu moja ni kupeperusha bendera za mataifa tofauti''.
Waziri huyo amesema kuwa malalamishi yametumwa katika serikali ya Korea Kaskazini wakilaumu biashara hiyo ya ujanja.
''Shirika la kimataifa la maswala ya baharini pia limeelezewa ili kuwakamata wamiliki wa meli hizo'',aliongezea Mahiga.