Taifa la Burundi hatimaye limekuwa taifa la kwanza kujiondoa rasmi katika mkataba wa Roma unaosimamia mahakama ya kimataifa kuhusu uhalifu wa kivita ICC.
Hatua hiyo inajiri baada ya rais wa taifa hilo Pierre Nkurunziza kutia saini sheria iliopitishwa na bunge pamoja na seneti ya kuiondoa Burundi katika mkataba huo.
Wiki iliopita ,bunge la Burundi liliidhinisha mpango wa baraza la mawaziri kukata uhusiano na mahakama hiyo ya mjini Hague.
Tayari mahakama ya ICC imeitaja mipango ya Burundi ya kujiondoa katika mahakama ya kimataifa kuhusu uhalifu wa kivita ICC kuwa 'pigo' katika vita dhidi ya watu wasioheshimu sheria.

Barua iliotiwa saini na rais Nkurunziza kuiondoa Burundi katika ICC
Image captionBarua iliotiwa saini na rais Nkurunziza kuiondoa Burundi katika ICC

Mwendesha mashtaka wa ICC alinukuliwa akisema kuwa atachunguza kile kilichotokea Burundi wakati wa maandamano dhidi ya rais Pierre Nkurunziza.
Aliyekuwa waziri wa haki nchini Senegal Sidiki Kaba,ambaye anaongoza bodi hiyo ya ICC ,alitoa wito kwa Burundi kuzungumzia wasiwasi wake badala ya kujiondoa katika mahakama hiyo.
Mwaka uliopita,marais wa Umoja wa Afrika walipitisha pendekezo kutafuta njia ambayo bara la Afrika lingeweza kujiondoa katika mahakama hiyo kwa pamoja.
Kumekuwa na malalamishi kwamba mahakama hiyo inalenga maswala ya Afrika pekee.
Kesi zote zinazoangaziwa na mahakama hiyo zinatoka Afrika.