CHUO cha Usafirishaji Tanzania (NIT) jijini Dar es Salaam kimetakiwa kuboresha idara yake ya ukaguzi wa magari kwa ajili ya kukijengea uwezo wa kufanya kazi hiyo.
Agizo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Miundombinu, Profesa Norman Sigalla baada ya kamati hiyo kusikiliza na kujadili taarifa ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kuhusu utendaji kazi wa NIT na Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI).

Ameitaka wizara hiyo kusimamia maboresho ya miundombinu kwenye vyuo vya NIT na DMI ili viwe na hadhi kulingana na umuhimu wake kwa taifa.
"Tunataka vyuo hivi viwe na wataalamu wenye uwezo kabla ya kupewa haki ya kufundisha ili viweze kuzalisha wataalamu wazuri wakiwemo mabaharia watakaochangia maendeleo na watakaoweza kujiajiri," amesisitiza.
Ametoa changamoto kwa vyuo hivyo vijikite kwenye utafiti na kutoa machapisho yenye lengo la kutatua matatizo yanayolikabili taifa.
“Kamati inahitaji taarifa iliyokamilika ya ujenzi wa reli ya kati katika kipindi cha kuanzia sasa na Novemba 14, mwaka huu, tumeiagiza wizara itekeleze agizo hili,” amesema.