Rais wa Ufilipino, Rodrigo Duterte, amesema kuwa ameagiza kufutiliwa mbali kandarasi ya kununua maelfu ya bunduki kutoka Marekani.
Bw Duterte amesema kuwa taifa lake litatafuta njia mbadala ya kununua silaha hizo kwingine kwa bei nafuu.

Idara ya polisi ya Ufilipino ilikuwa imepangiwa kununua takriban bunduki 26,000 kutoka Marekani.
Uhusiano baina ya nchi hizo mbili ambazo zilikuwa washirika kwa muda mrefu, umedorora tangu Bw Duterte aingie madarakani.
Kumekuwepo taarifa kwamba Marekani ilikuwa tayari imepanga kutoiuzia Ufilipino silaha hizo, kutokana na wasiwasi kuhusu ukatili wa Bw Duterte hasa katika kukabiliana na walanguzi wa dawa za kulevya.
Watu wanaotuhumiwa kuhusika katika ulanguzi wa mihadarati wamekuwa wakipigwa risasi na kuuawa.