MFANYAKAZI wa ndani wa Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Angella Kizigha, Miraji Mkanga (41) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam kwa madai ya umwibia mwajiri wake vitu ikiwemo bastola yenye risasi 23, simu, mikufu na bangili za dhahabu, vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya Sh milioni 85.

Akisomewa mashitaka hayo na Karani Dayz Makalala mbele ya Hakimu Joyce Mushi, ilidaiwa kuwa mshitakiwa Mkanga alitenda kosa hilo Oktoba 2, mwaka huu maeneo ya Kijitonyama wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Makakala alidai mtuhumiwa huyo aliiba Dola za Marekani 3,500 zenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 7.5, bangili za dhahabu gramu 300 zenye thamani ya Sh milioni 36, hereni gramu 450 zenye thamani ya Sh milioni 42, doti 30 za vitenge zenye thamani ya Sh milioni 1.5 na shuka 10 zenye thamani ya Sh 700,000.
Aidha, mfanyakazi huyo wa ndani anatuhumiwa kuiba bastola moja iliyotengenezwa Jamhuri ya Czech yenye namba No B 283994 na risasi 23 thamani ya Sh milioni mbili, simu mbili za Samsung zenye thamani ya Sh 500,000 na nguo tofauti zenye thamani ya Sh 750,000 mali ya mbunge huyo ambaye ni kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Mshitakiwa alikana shitaka hilo wakati huo dhamana yake ipo wazi, akitakiwa kuwa na wadhamini wawili kutoka katika taasisi inayotambulika na kusaini hati ya dhamana ya Sh milioni tano kila mmoja.
Kesi hiyo inatarajiwa kutajwa tena Novemba 28, mwaka huu, na mshitakiwa alirudishwa rumande kutokana na wadhamini wake kutofika huku upelelezi ukiendelea.
Wakati huo huo, Mwandishi Wetu Flora Mwakasala anaripoti kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachia huru Mbunge wa Sumve mkoani Mwanza, Richard Ndassa (56) aliyekuwa anakabiliwa na mashitaka ya kuomba rushwa ya Sh milioni 30. Ndassa aliachiwa huru jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Victoria Nongwa. Aliachiwa huru baada ya kuonekana hana kesi ya kujibu.
Katika mashtaka yake, Ndassa alikuwa anadaiwa kuomba rushwa hiyo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Felchesmi Mramba.
Awali akisomewa mashtaka ilidaiwa Machi 13, mwaka huu, Dar es Salaam, mshtakiwa akiwa Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji aliomba rushwa ya Sh milioni 30 kutoka kwa Mramba ili kamati hiyo itoe hati safi ya ukaguzi wa ripoti ya hesabu za mwaka 2015/2016 kwa shirika hilo la umma.
Iliendelea kudaiwa mahakamani hapo kuwa, siku hiyo hiyo Dar es Salaam, mshtakiwa alimshawishi Mramba amuunganishie umeme ndugu yake Ndassa, Matanga Mbushi na rafiki yake Lameck Mahewa ili kamati yake itoe hati safi ya ukaguzi wa ripoti ya hesabu ya mwaka 2015/2016 kwa shirika hilo.