SERIKALI imeombwa kutengeneza bajeti ya kusaidia taasisi mbalimbali zinazojishughulisha na kusaidia watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI ikiwa ndio njia ya kuhakikisha huduma kwa waathirika hao zinaendelea kuimarika.

Imeelezwa kuwa ingawa serikali ndiyo inayotoa dawa za kufubaza makali ya UKIMWI ARVs, haitengenezi bajeti kwa ajili ya wafanyakazi wanaohudumia waathirika kisaikolojia na kitiba.

Hoja hiyo imetolewa na Meneja mradi wa Pastoral Activities and Services for People with AIDS Dar es Salaam Archdiocese (PASADA) Jovin Riziki wakati akijibu maswali katika mkutano na ujumbe wa nchi za jumuiya ya NORDIC waliotembelea makao makuu ya PASADA yaliyopo Chang’ombe, Temeke Dare s salaam kuangalia miradi mbalimbali ya kijamii inayofadhiliwa na UNICEF.

Nchi za Jumuiya ya Nordic ni wafadhili wakubwa wa miradi inayoendeshwa na Mashirika ya Umoja wa Mataifa hapa nchini.
Meneja mradi wa Pastoral Activities and Services for People with AIDS Dar es Salaam Archdiocese (PASADA) Jovin Riziki (kushoto) akitoa maelezo kwa sehemu ya ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana mwenyeji wao Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez (wa pili kulia) katika chumba cha kuhifadhia kumbukumbu za wagonjwa ulipotembelea kwenye kituo hicho cha PASADA jijini Dar es Salaam. Kulia ni kiongozi wa ushirikiano wa kimataifa wa Shirika la Misaada la Sweden (SIDA), Anders Rönquist.(Habari picha na Zainul Mzige wa Modewjiblog)

Akijibu swali nini ambacho atataka kumweleza Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akikutana naye, Riziki alisema kwamba angelipenda kuona serikali inawajibika kusaidia huduma katika taasisi mbalimbali zinazoigusa jamii zinaendelea kutolewa.

Alisema asasi zinazosaidia waathirika wa UKIMWI kama hiyo ya PASADA hutegemea asilimia 100 misaada ya nchi na wafadhili wa kigeni ambapo miradi ikimalizika mara nyingi waliokuwa wanahudumiwa hukosa mahali pa kupata misaada iliyokuwa inawawezesha kuendelea kuishi kiutu kwa kuwa na siha njema na kufanya shughuli za kiuchumi.
Meneja mradi wa Pastoral Activities and Services for People with AIDS Dar es Salaam Archdiocese (PASADA), Jovin Riziki (kushoto) na ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana mwenyeji wao Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez (kulia) wakipata maelezo kutoka kwa mtoa huduma katika kitengo cha dawa za kupunguza makali ya Virusi vya UKIMWI ARV's ulipotembelea kwenye kituo hicho cha PASADA jijini Dar es Salaam.

Alisema kuna changamoto kubwa kuhudumia wagonjwa zaidi ya elfu 21 wengine wakiwa kufani majumbani bila kuwa na mtaji wa kutosha hasa malipo kwa watoa huduma ambao ni wataalamu.

“Ipo haja ya serikali kuchangia kazi hii ya kibinadamu hasa fedha kwa ajili ya kulipa wataalamu na kuendeleza miradi ambayo inasaidia jamii moja kwa moja” alisema huku akiongeza kwamba kwa sasa mathalani wanaendelea kufanya mazungumzo na watu mbalimbali kuendeleza mradi uliokuwa ukisaidiwa na USAID.

Alisema Septemba mwaka huu USAID wamemaliza mchango wao wa mradi muhimu ambao ndani yake ulikuwa unawasaidia waathirika katika elimu, tiba na pia kiuchumi.
Ujumbe huo ukiwa kwenye mazungumzo na vijana wanaoishi na VVU ambao wamepata mafunzo ya ujasiriamali yaliyowawezesha kujiajiri kwa kufanya biashara ndogo ndogo zinazowapatia kipato cha kusaidia familia zao na mahitaji yao madogo madogo.

Alisema mara nyingi kunapoendeshwa mradi ambao ndani yake watu wanawezeshwa kiuchumi hujitokeza kwa wingi na hivyo kama serikali ikitenga bajeti maana yake watu hao watafika kupata elimu na pia kufufua matumaini ya maisha kwa kuwezeshwa kiuchumi.

PASADA iliyoanza Agosti 1992 wakati kundi dogo la watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI kujikusanya ili kupata msaada wa pamoja sasa hivi ina wateja 36,000, ikitoa huduma za upimaji kwa watu 10,000 kila mwezi.

Aidha PASADA ambayo imekuwa ikikua ikitegemea fedha za wahisani imekuwa ikiwafikia watu walio majumbani ambao hawawezi na waliokufani kuwapatia huduma za kibinadamu.
Ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana mwenyeji wao Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez (hayupo pichani) wakipata maelezo nje ya eneo la vipimo katika kituo cha PASADA.

Ingawa PASADA ipo chini ya kanisa katoliki huduma zake hupatikana kwa kila mwananchi bila ubaguzi na huendesha pia huduma za elimu kuhusu afya ya uzazi, ujana na maradhi ya UKIMWI.

Sehemu kubwa ya elimu ni kuondoa unyanyapaa na kuhimiza wananchi kupima afya zao. Aidha elimu imelenga watu kubadilika tabia.

Ikiwa na watu wazima 3000 wanaotumia dawa na watoto 600, PASADA imesema kwamba bado inakabiliwa na changamoto kubwa hasa pale ambapo wahisani wanapojitoa kusaidia miradi iliyopo ya elimu na kiuchumi.

Aidha PASADA imekuwa ikipambana kwa kusaidiana na wadau wengine kuhakikisha kwamba haki za msingi za wenye virusi vya UKIMWI hazikiukwi.
Meneja mradi wa Pastoral Activities and Services for People with AIDS Dar es Salaam Archdiocese (PASADA), Jovin Riziki akiongoza ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana watalaam kutoka mashirika ya Umoja wa Mataifa pamoja na mwenyeji wao Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez (wa pili kulia) kutembelea vitengo mbalimbali vinavyotoa huduma kituo cha PASADA jijini Dar es Salaam.

Ikiwa imefanikiwa kupunguza maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kwa asilimia 97, huku ikiwa imefikia asilimia 4 ya waathirika nchini na kwa mikoa ya Dar es salaam na Pwani asilimia 30, PASADA ikiwa na wafanyakazi 140 inahitaji sana uhakika wa bajeti na serikali ndiyo inayoweza kutoa kwa kuwa kazi inayofanywa na serikali kupitia vituo vya umma ndiyo inafanywa na PASADA.

Ujumbe huo wa NORDIC ambao ulikujwa na wenyeji wao Mashirika ya Umoja wa Mataifa ulielezea kuridhishwa kwake na kazi inayofanywa na PASADA na kusema ipo haja kwa wadau kushirikiana kurejesha heshima ya binadamu na kufanya serikali kuwajibika kwa watu wake.

Naye Mratibu Mkazi wa mashirika ya Umoja wa Mataifa ambaye ndiye mwenyeji wa ujumbe huo unaopita katika miradi mbalimbali serikalini na hata katika taasisi binafsi, Alvaro Rodriguez, alisema kuna changamoto nyingi katika kusaidia wananchi katika maradhi yanawasibu kwa sababu ni kazi ya kibinadamu zaidi na wala si ya kimaendeleo.
Ziara ya ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana watalaam kutoka mashirika ya Umoja wa Mataifa ikiendelea kutembelea vitengo mbalimbali vinavyotoa huduma za afya kwa watu wanaoishi na VVU kituo cha PASADA jijini Dar es Salaam.

Alisema hata hivyo ili kuwa na haki sawa mashirika ya Umoja wa Mataifa yamekuwa yakisaidia kupatikana kwa haki za maisha kwa kusaidia mambo kadhaa ambayo hayana uhusiano wa moja kwa moja na wagonjwa lakini yakiwa na mchango mkubwa katika afya na shughuli za uzalishaji mali.

Alisema amefurahishwa na ziara ya ujumbe huo wa Nordic ambao ni wafadhili wakubwa wa miradi mbalimbali yenye lengo la kuwezesha uwajibikaji na utawala bora nchini ikiwemo misaada ya kibinadamu.

Alisema ni kazi ya mashirika ya Umoja wa Mataifa kushawishi mabadiliko ya kitamaduni ili kujiweka sawa katika shughuli za maendeleo.
Ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana watalaam kutoka mashirika ya Umoja wa Mataifa ukiwa katika eneo maalum lililotengwa na kituo cha PASADA kwa ajili ya watoto kufanya michezo mbalimbali walipofanya ziara kituoni hapo. 
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez (kulia) akibadilishana mawazo na kiongozi wa ushirikiano wa kimataifa wa Shirika la Misaada la Sweden (SIDA), Anders Rönquist wakati wa ziara ya kutembelea vitengo mbalimbali katika kituo kinachohudumia watu wanaoishi na VVU, PASADA jijini Dar es Salaam.
Meneja mradi wa Pastoral Activities and Services for People with AIDS Dar es Salaam Archdiocese (PASADA), Jovin Riziki akitoa historia fupi ya kituo hicho pamoja na changamoto zinazowakabili katika kuhudumia watu wanaoishi na VVU nchini kwa ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana watalaam kutoka mashirika ya Umoja wa Mataifa ulipotembelea kituo hicho.
Sehemu ya ujumbe huo ukimsikiliza Bwana Jovin Riziki.
Kiongozi wa ushirikiano wa kimataifa wa Shirika la Misaada la Sweden (SIDA), Anders Rönquist akifafanua jambo wakati wa kutoa mrejesho baada ya ziara ya kutembelea vitengo mbalimbali katika kituo cha PASADA jijini Dar es Salaam.
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa PASADA baada ya ziara ya kutembelea kituo hicho na kujionea changamoto zinazowakabili.